Watanzania jengeni utamaduni wa majadiliano ili kudumisha misingi ya haki, amani,
upatanisho na umoja wa kitaifa!
Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania anabainisha kwamba, Kanisa
linatambua na kuthamini misingi ya haki, amani na upatanisho katika maisha na maendeleo
ya watu.
Kwa bahati
mbaya katika Jamii kuna watu ambao kwa makusudi mazima au kwa kutoelewa kwao wameshindwa
kuthamini amani na utulivu nchini Tanzania. Matokeo yake ni: malumbano, kinzani na
choko choko za kidini zinazofanywa na waamini wenye misimamo mikali ya kiimani.
Mazingira
kama haya yanaweza kuwajengea baadhi ya watu hisia za chuki, uhasama na hali ya kutaka
kulipiza kisasi. Kanisa bado linaendelea kuwahamasisha waamini na watanzania wenye
mapenzi mema kujikita katika kutafuta na kudumisha misingi ya haki, amani, upatanisho
na umoja wa kitaifa kwa ajili ya mafao ya wengi. Kamwe wasiingie kwenye kishawishi
cha kutaka kulipiza kisasi, kwani vita haina macho, watakaoathirika zaidi ni wale
watu ambao hawana hatia.
Kuna haja kwa watanzania anasema Askofu mkuu Josephat
Lebulu kujikita katika majadiliano ya kidini na kiekumene, wote wapanie kutafuta amani
na upatanisho kwani ni heri wapatanishi maana wao wataitwa ni wana wa Mungu. Watanzania
watafute mambo yanayopelekea chokochoko na kinzani za kidini; tofauti zao za kimsingi
na kubainisha hatua ambazo zinaweza kuchukuliwa ili kuendeleza misingi ya haki, amani
na utulivu nchini Tanzania. Wananchi washinde ubaya kwa kutenda wema.
Askofu
mkuu Josephat Lebulu akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni kuhusu Maadhimisho
ya Jubilee ya Miaka 50 ya Ukristo Jimbo kuu Katoliki Arusha, alisema, Kanisa katika
mikakati yake linapenda kutumia fursa hii kusali kwa ajili ya kuombea amani, utulivu
na upatanisho wa kweli. Maadhimisho ya Jubilee ya Ukristo yanakwenda sanjari na Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa na hatimaye, kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, changamoto ya kumwilisha imani katika matendo.
Waamini kwa
wakati huu watatembeza Msalaba wa Jubilee katika Familia, Jumuiya na Parokia zote
za Jimbo kuu la Arusha. Kilele cha Maadhimisho ya Jubilee hii ni hapo Desemba 2013.
Ni matumaini ya Askofu mkuu Lebulu kwamba, Kanisa kuu la Jimbo kuu la Arusha litakuwa
limekamilika na waamini wataweza kusali humo ili kumshukuru Mungu kwa zawadi ya imani.
Jimbo kuu la Arusha lina matatizo, fursa na changamoto ambazo linaendelea kuzifanyia
kazi katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo, ili kuhakikisha kwamba, Uinjilishaji
wa kina unagusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.