Rais wa Makanisa ya Kiinjili ya Kiluteri nchini Ujerumani akutana na kuzungumza na
Papa Francisko mjini Vatican
Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu amekutana na kuzungumza na na Mheshimiwa Nikolaus
Schneider, Rais wa Makanisa ya Kiinjili ya Kiluteri nchini Ujerumani.
Akizungumzia
tukio hili, Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Mheshimiwa
Schneider, amempongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa kuchaguliwa kwake kuliongoza Kanisa
na kwa namna ya pekee, jina ambalo ni kama dira na mwongozo wa maisha na utume wake
kama Khalifa wa Mtakatofu Petro kwani jina la Mtakatifu Francisko wa Assisi ni jina
lenye mvuto na mashiko kwa Wakristo wengi sehemu mbali mbali za dunia.
Viongozi
hawa wawili wamezungumzia pia shida na mahangaiko ya wananchi wa Argentina waliokumbwa
na mafuriko hivi karibuni na kusababisha maafa makubwa, jambo ambalo limewagusa viongozi
hawa wawili na kuonesha moyo wa mshikamano na upendo kwa wote walioathirika.
Majadiliano
ya kiekumene yamelenga zaidi ushuhuda wa imani unaooneshwa na wafiadini wa Kikristo
kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Viongozi hawa wanatambua mateso na mahangaiko
ya waamini wao walioteswa na kudhulumiwa nyakati za tawala za kidhalimu.
Wanasema,
damu ya mashahidi hawa wa imani ni jambo linalowaunganisha Wakristo kutoka Makanisa
mbali mbali ili kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Kanisa la
Kiinjili la Kiluteri linajiandaa kuadhimisha tukio la kihistoria la mageuzi ndani
ya Kanisa litakalofanyika kunako mwaka 2017.
Papa Francisko amekumbushia hotuba
ya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI aliyoitoa mjini Erfurt, mahali alipozaliwa
na Martin Luther na kutekeleza utume wake ndani ya Kanisa, changamoto ya kuendeleza
majadiliano ya kiekumene baina ya Makanisa haya mawili mintarafu mapokeo ya Mageuzi
yaliyoletwa na Martin Luther. Mazungumzo baina ya viongozi hawa wawili anasema Padre
Lombardi yamekuwa na manufaa makubwa baina ya Makanisa haya mawili.