2013-04-08 08:41:36

Familia za Kikristo katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani


Tangu Baba Mtakatifu Francisko alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, kumekuwepo upepo tofauti unaovuma kukazia umoja, upendo na mshikamano wa dhati; imani na matumaini kwa wale waliokata tamaa pamoja na ushuhuda wenye mvuto kwa Kristo na Kanisa lake. RealAudioMP3
Ni maneno ya Askofu Mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia katika hafla fupi ya maboresho ya tovuti ya Baraza lake na Jarida ambalo linatolewa katika lugha nne za kimataifa kwa ajili ya Familia, kama sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Nane ya Familia Kimataifa, itakayofanyika Jijini Philadelphia, kuanzia tarehe 22 hadi tarehe 27 Septemba 2015.
Hili ni tukio la Kikanisa linalozihusisha familia za kikristo katika maisha na utume wake. Familia kutoka sehemu mbali mbali za dunia zimeanza pia maandalizi kwa ajili ya kushiriki katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa kuungana na Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 26 hadi 27 Oktoba 2013 ili kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa zawadi kubwa ya Familia. Itakuwa ni fursa kwa familia hizi kuweza kuimaarisha imani yao kwa kutembelea Makaburi ya Miamba wa Imani hapa Mjini Roma.
Katika mkutano wa Baraza la Kipapa la Familia uliofanyika hivi karibuni, baadhi ya wajumbe walionesha kuguswa na mtindo wa maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko hadi sasa, lakini pia wakaonesha wasi wasi wao kuhusu changamoto mbali mbali anazopaswa kukabiliana na zo katika kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia. Wanasema, bado ulimwengu wa wanasiasa unaendelea kumsoma kwa umakini mkubwa; hali ya kutovumiliana pamoja na utengenezaji wa sera ambazo kimsingi zimekuwa na ukakasi mkubwa katika maisha na utume wa Familia katika Jamii.
Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, Kardinali Jorge Bergoglio amekuwa ni rejea makini ya miakati ya kichungaji, maisha adili na utu wema nchini Argentina. Ni kiongozi ambaye anatoka katika kundi la Mapadre vijana kutoka Amerika ya Kusini waliokuwa na ari, moyo na shauku ya kuleta mabadiliko: kiroho na kimwili, kwenye miaka ya sitini na sabini; matunda ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, moto wa kuotea mbali!
Ni Kiongozi aliyesimama kidete kulinda na kuwatetea wanyonge waliokuwa wanaelemewa na athari za myumbo wa uchumi nchini Argentina; hali iliyopelekea idadi kubwa ya wananchi wa Argentina kuikimbia nchi yao na kuhamia ugenini ambako walijikuta wakiwa ni wahamiaji.
Baba Mtakatifu Francisko ni kiongozi ambaye hadi sasa kwa maneno na matendo yake ni Baba mwenye huruma anayesahihisha, anayetangaza na kukanya pale watoto wake wanapoonekana kutaka kuteleza na kuanguka katika utupu wa mawazo na maisha! Uwepo wake ni kielelezo cha mwanga angavu wa matumaini kwa watu waliokuwa wamekata tamaa.
Huyu ndiye yule Msamaria mwema anayeguswa na mahangaiko ya jirani zake, kiasi kwamba, anajishusha ili kuwaganga kwa neno la faraja na uwepo wake unaoleta mguso!
Kardinali Bergoglio anakumbukwa na watu wengi nchini Argentina kama kiongozi aliyesimama kidete kulinda na kutetea: amani, utulivu, haki msingi za binadamu na mafao ya wengi. Daima alipenda kusimamia utawala wa sheria na kila mtu kuthaminiwa ili kuondokana na wasi wasi zisizo na msingi. Mtindo huu wa maisha na utume kwa Kanisa, Kardinali Bergoglio ameacha deni kubwa kwa viongozi mbali mbali nchini Argentina.
Ni matumaini ya wajumbe wa mkutano wa Baraza la Kipapa la Familia kwamba, ile dhamana ambayo Wakristo na watu wengi wenye mapenzi mema wameonesha kwa kutaka kusali na kumwombea wataweza kutekeleza wajibu wao, ili kweli Baba Mtakatifu Francisko aweze kutekeleza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa ufanisi mkubwa kadiri ya mapenzi ya Mungu mwenyewe.








All the contents on this site are copyrighted ©.