2013-04-06 08:43:26

Papa Tawadros II aonesha nia ya kukutana na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican


Patriaki Tawadros wa pili wa Kanisa la Kikoptik la Kiorthodox la Alexandria, Misri ameonesha nia na utashi wa kutaka kukutana na Baba Mtakatifu Francisko kama sehemu ya mchakato wa kuendeleza majadiliano ya kiekumene baina ya Makanisa haya mawili. Hayo yamenukuliwa hivi karibuni na vyombo vya habari kutoka Misri.

Papa Tawadros wa pili, hivi karibuni alikutana na kuzungumza na Askofu mkuu Jean Paul Gobel, aliyeteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kuwa Balozi wa Vatican nchini Misri. Katika mazungumzo ya viongozi hawa wawili, Papa Tawadros wa pili alionesha nia ya kutaka kusafiri hadi mjini Vatican ili kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko, ili kujenga na kuimarisha mshikamano wa kidugu baina ya Makanisa haya mawili.

Ikiwa nia hii njema itaweza kutekelezwa, basi hili litakuwa ni tukio kuu la Kiekumene kuwahi kutokea tangu mwaka 1973, wakati ambapo Papa Shenuda wa Tatu, alipokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Paulo wa sita mjini Vatican. Viongozi hawa wawili katika mazungumzo yao walitoa tamko la pamoja kuhusiana na uelewa wa mafundisho juu ya Yesu na tangu hapo wakaanzisha mchakato wa majadiliano ya kiekumene baina ya Makanisa haya mawili.







All the contents on this site are copyrighted ©.