2013-04-06 12:05:29

Mheshimiwa Padre Josè Rogriguez Carballo ateuliwa na Papa kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Mheshimiwa Padre Josè Rodriguez Carballo, Mkuu wa Shirika la Ndugu Wadogo wa Mtakatifu Francisko kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume pamoja na kumpandisha hadhi kuwa ni Askofu mkuu.

Askofu mkuu mteule alizaliwa tarehe 11 Agosti 1953 nchini Hispania. Baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa na kipadre, akapadrishwa kunako tarehe 28 Juni 1977 mjini Yerusalemu kwenye Kanisa la Mtakatifu Salvatori. Baada ya Upadrisho aliendelea na masomo ya Sayansi ya Maandiko Matakatifu mjini Yerusalemu na Roma na kubahatika kupata shahada ya Uzamivu katika Maandiko Matakatifu kunako mwaka 1981.

Tangu wakati huo ametekeleza utume wake katika medani mbali mbali za maisha ya kitawa kama: Mlezi wa Wanovisi, Mchumi, Katibu mkuu wa majiundo, Gombera, Jaalim. Kati ya mwaka 1992 hadi mwaka 1997 alikuwa ni Mkuu wa Kanda na Rais wa Wakuu wa Shirika la Wakapuchini Barani Ulaya. Kunako mwaka 2003 akachaguliwa kuwa Mkuu wa Shirika la Wakapuchini na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Antonianum, kilichoko mjini Roma. Mwaka 2012 alichaguliwa kuwa Rais wa Shirikisho la Wakuu wa Mashirika ya Kitawa Duniani.

Hadi uteuzi wake, alikuwa ni mwanachama wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu, Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume na amekuwa mshiriki mzuri katika Maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu zilizofanyika kunako mwaka 2005, 2008, 2012 pamoja na Sinodi Maalum ya Maaskofu Katoliki Mashariki ya Kati, iliyoadhimishwa mjini Vatican kunako mwaka 2010.

Askofu mkuu mteule Josè Rodriguez Carballo ni mwandishi maarufu wa vitabu na majarida kuhusu maisha ya kuwekwa wakfu, Taalimgu uchungaji, Maandiko Matakatifu na Tasaufi ya Wafranciskani pia ni mtaalam aliyebobea katika lugha mbali mbali za kimataifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.