2013-04-05 09:25:03

Wakora Ta Nestor Timanywa, karibu Askofu Rwoma Jimboni Bukoba!


Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro anamshukuru na kumpongeza Askofu mstaafu Nestor Timanywa wa Jimbo Katoliki Bukoba kwa kazi kubwa ya kitume aliyoifanya kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa Familia ya Mungu Jimbo Katoliki Bukoba, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na kwa watanzania wote waliobahatika kupata huduma yake kama Askofu. RealAudioMP3

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu Mkude anakiri kwamba, kunako mwaka 1975 walipokutana kwa mara ya kwanza, alishangaa kumwona Askofu kijana kabisa katika maisha yake na Askofu Timanywa alimwomba ili aweze kumwombea kwa Mungu amsaidie katika maisha na utume wake kama Askofu.

Ni kiongozi ambaye ameonesha unyofu, utaratibu na kwamba, Askofu Timanywa kwa hakika ni mtu wa watu. Kanisa linamshukuru na kumpongeza kwa utume wake na kwa sasa anastahili kupumzika ili aweze kupata muda zaidi wa kusali na kutafakari kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa Jimboni Bukoba.

Askofu Mkude anasema, wanafahamiana vizuri na Askofu Rwoma wa Jimbo katoliki Bukoba na Msimamizi wa kitume wa Jimbo Katoliki Singida. Askofu Rwoma ambaye enzi zake alikuwa ni mchezaji mahiri wa mpira wa miguu, sasa kwa unyenyekevu mkubwa amejiweka kuwa ni mpira wa Mungu.

Anampongeza kwa kuteuliwa kuliongoza Jimbo Katoliki Bukoba ambalo ni kubwa na lina waamini na changamoto nyingi, ikilinganishwa na Jimbo Katoliki Singida. Jambo la msingi ni kujipa moyo, kila jambo linawezekana kwa mtu mwenye imani thabiti, bidii na utashi wa kusonga mbele kwa kasi na ari kubwa zaidi.

Askofu Mkude anawaalika Watu wa Mungu Jimbo Katoliki Bukoba, kutoa ushirikiano mkubwa kwa Askofu Rwoma, kwani ni mtu mwenye mipango, jasiri na Mchamungu. Ameteuliwa kwa kazi maalum na kwa wakati maalum kwa ajili ya Jimbo Katoliki Bukoba.







All the contents on this site are copyrighted ©.