2013-04-05 12:19:44

Viongozi wa kitaifa, wekeni bayana sera na mikakati ya kupambana na baa la njaa nchini mwenu!


Bwana Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO, amewataka viongozi wa kitaifa kuhakikisha kwamba, wanatekeleza wajibu wao msingi, ili watu wao waweze kuwa na uhakika na usalama wa chakula mara baada ya kuhitimisha mikakati ya Malengo ya Maendeleo ya Millenia hapo mwaka 2015. Serikali zinapaswa kujipanga kikamilifu ili kupambana na baa la njaa ambalo bado limekuwa ni tishio kwa maisha ya watu wengi duniani.

hadi sasa kuna dalili za maendeleo yaliyokwishafikiwa katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia, lakini bado kuna watu zaidi ya millioni 870 wanaokabiliwa na baa la njaa. Mikakati ya kuwa na uhakika wa usalama wa chakula bado haijapata mafanikio ya kutosha, kumbe kuna haja kwa viongozi wa Kitaifa kujipanga vyema ili kukabiliana na changamoto hii, kwa kutambua kwamba, chakula ni sehemu ya haki msingi za binadamu, jambo linalohitaji sera makini kwa siku za usoni.

Bwana Josè Graziano da Silva ameyasema hayo siku ya Alhamisi tarehe 4 Aprili 2013 alipokuwa anazungumza na wajumbe wa ngazi za juu uliokuwa unajadili taswira ya Umoja wa Mataifa baada ya Mwaka 2015. Anasema, Jumuiya ya Kimataifa ina uwezo wa kuzalisha chakula cha kutosha kwa watu wengi, kumbe, jambo la msingi kwa wakati huu ni kuhakikisha kwamba, kunakuwepo na maboresho ya lishe katika ngazi za vijijini.

Juhudi hizi hazina budi kwenda sanjari na uwekezaji katika shughuli za kilimo na uzalishaji vijijini, mahali ambapo asilimia 70 ya watu wanaokabiliwa na njaa wanaishi; sehemu ambako wananchi wengi wanategemea kilimo kwa ajili ya maisha yao kwa kutoa ajira ya watu zaidi ya millioni 500. Mkakati huu hauna budi kuungwa mkono na sera makini za uchumi wa dunia; amani na utulivu, kwani kinzani na migogoro imepelekea kushuka kwa uzalishaji katika sekta ya kilimo.

Kuna haja pia ya kulinda na kutunza mazingira pamoja na rasilimali za nchi. Juhudi hizi zinapaswa kutekelezwa kwa mshikamano wa dhati kati ya nchi husika na Jumuiya ya Kimataifa.









All the contents on this site are copyrighted ©.