2013-04-05 08:07:51

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Huruma ya Mungu


Katika furaha ya Pasaka, tunaendelea kuzitangaza sifa za Bwana kwa mataifa yote, tukiwa tayari Dominika ya II ya Pasaka mwaka C. Neno la Mungu linatufundisha kuitazama Jumuiya ya Kwanza iliyohuishwa na Neno la Mungu kama hakiki ya kwamba Yesu Kristu amefufuka na anaishi. RealAudioMP3

Mwinjili Yohane anakazia Imani, zaidi ya kuona, Bwana akisema wa heri wanaosadiki bila kuona. Mwinjili anasonga mbele akiweka mbele yetu ungamo la imani la Mtakatifu Thoma Mtume ambaye mwanzoni alionesha hali ya kutokuamini mpaka awe amegusa makovu ya Bwana!

Bwana akishawatokea Mitume waliokuwa wamekusanyika pamoja na kuwatakia amani ambalo ni tunda la ufufuko atawavuvia Roho Mtakatifu ili wapate kuondolea dhambi, wapate kukabiliana na nguvu za giza. Ni katika siku hii Yesu Kristo mfufuka anaweka sakramenti ya Kitubio.

Jambo moja la kukumbuka katika siku zetu hizi ni kujua kuwa, Roho Mtakatifu ni amani na wala si ugomvi na vurugu katika maisha yetu. Tuwe makini na shughuli mbalimbali amabazo hufanywa katika madai yakwamba tumetumwa na Roho Mtakatifu. Ni lazima nyuma yake kutanguliwe na amani na kisha kumalizike na amani.

Mpendwa mwana pasaka Bwana anawatokea mitume wakiwa wamekusanyika katika jumuiya na anawapatia salamu yake maarufu sana yaani “amani iwe kwenu”. Mara moja Bwana anataka kusisitiza maisha ya jumuiya na hivi ni katika jumuiya twaweza kusikia na kusikiliza Neno na salaamu ya Mwenyezi Mungu. Ni kwa jinsi hiyo basi asiyekuwepo katika jumuiya hawezi kuipata salaamu hiyo na kusikia Neno la Mungu.

Bwana anapotoa salaam hiyo anaifungamanisha na furaha, Roho Mtakatifu na amani kumbe jumuiya ni kitovu cha Roho Mtakatifu na amani. Leo hii tunazo jumuiya ndogondogo, tunalo kusanyiko la Ekaristi Takatifu Dominika na siku nyingine, tuanayo mikutano ya Halmashauri, kwaya hivi vyote ni nafasi mwanana kwa ajili ya kupokea neema za Mungu kwa njia ya Roho Mtakatifu, kumbe yafaa tuviadhimishe kwa ustadi na upendp mkubwa.

Mtume Thoma ambaye anataka kuona ndipo aamini ni kielelezo cha mateso na hofu ya Mitume kabla ya kuamini ufufuko wa Bwana. Kwa hakika haikuwa rahisi kwa Mitume kuamini pamoja na matokeo ya mbalimbali ya Bwana lakini polepole watafikia kilele cha imani. Katika hili Mwinjili anataka kuwasaidia waamini ambao walipenda kuona kabla ya kuamini, kwamba Kristu mfufuka hafungwi na milango ya ufahamu bali anaonekana kwa imani.

Na kwa hakika imani haipatikani katika kile tunachokiona, kumbe anayetaka kugusa na kuona hawezi kuwa na imani. HERI WASIOONA NA WAKAAMINI. Tena haya yameandikwa ili tuweze kusadiki na kuamini, na kwa namna hiyo hakuna njia nyingine ya kusadiki isipokuwa kwa njia ya NENO LA MUNGU. Kondoo wangu huijua sauti yangu,Yn 10:14,17 na hivi sauti ya Kristu husikika katika Injili yake.

Katika somo la kwanza kutoka katika Kitabu cha Matendo ya Mitume tunapata maelezo ya maisha ya Jumuiya ya kwanza huko Yerusalemu, jumuiya ambayo chimbuko lake ni Imani katika Yesu mfufufka. Kwa sababu ya imani waliyoipokea Mitume na kuiishi, Jumuiya ya Waamini ilizidi kuongezeka. Mitume waliwaponya watu shida zao mbalimbali, waliwahubiria Neno la Mungu na hili lilitokana na uhakika wao kwamba Bwana anaishi. Waamini waliongezeka kwa sababu Mitume walifanya alichofanya Bwana, nasi hivi tunaalikwa kufanya kilekile alichofanya Bwana.

Mpendwa mwana wa Mungu katika somo la pili katika kitabu cha ufunuo tunakutana na Mt. Yohane ambaye yuko katika kisiwa cha Patimo. Yuko huko kwa sababu ya imani yake katika Kristu mfufuka. Yuko uhamishoni, ni wakati wa Domisiani aliyetaka kuabudiwa kama Mungu na hivi Yohane anakataa! Mt. Yohane anataka kuwaimarisha wanaoteseka kwa sababu ya madhulumu wavumilie mateso yao wakitarajia furaha iliyo kuu yaani uzima wa milele.

Anatumia alama mbalimbali ambazo zataka kuleta ujumbe kwa waamini wanaoteswa. Ipo alama ya mwanadamu kati ya vinara 7, huyu ni Kristu mfufuka, vazi refu ni alama ya kuhani ambaye kwa sasa ni Kristo na wala hakuna mwingine, na hivi tumfuate yeye. Mshipi ambao amejifunga ni alama ya kifalme.

Mpendwa jambo ambalo Mt. Yohane ataka kulijenga ni kuwa Kristu mfufuka ndiye kitovu na dira ya maisha yetu, kumbe kila mmoja wetu ataweza kufika mbingu akipita kwa Bwana.

Nikutakie maisha ya Pasaka yaliyo ya furaha na zaidi tukikomaza Jumuiya Ndogondogo ambazo kwazo Kristo uhubiri Neno kila siku mpaka ukamilifu wa dahari. Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd. Richard Tiganya C.PP.S.









All the contents on this site are copyrighted ©.