2013-04-04 11:35:19

Ratiba elekezi za Ibada zitakazoadhimishwa na Papa Francisko mwezi Aprili-Mei 2013


Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa Monsinyo Guido Marini, ametoa ratiba elekezi ya Ibada zinazotarajiwa kuongozwa na Baba Mtakatifu Francisko katika kipindi cha Mwezi Aprili hadi Mwezi Mei, 2013.

Tarehe 7 Aprili 2013, Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Pasaka, maarufu pia kama Jumapili ya Huruma ya Mungu, Baba Mtakatifu Francisko, Saa 11:30 Jioni, atasimikwa rasmi kama Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Roma katika Ibada ya Misa Takatifu itakayofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, Makao Makuu ya Jimbo kuu la Roma.

Tarehe14 Aprili 2013, Jumapili ya Tatu ya Kipindi cha Pasaka, Baba Mtakatifu Francisko ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo, Nje ya Kuta za Roma, kuanzia Saa 11:30 Jioni.

Tarehe 21 Aprili 2013, Jumapili ya Nne ya Kipindi cha Pasaka, maarufu kama Jumapili ya Kristo Mchungaji mwema, Siku ya 50 ya Kuombea miito iliyoanzishwa na Papa Paulo wa sita na kwa mwaka huu inaongozwa na kauli mbiu "Miito mitakatifu ni alama ya matumaini yanayosimikwa katika imani. Hii itakuwa ni fursa muhimu kwa Baba Mtakatifu Francisko kutoa Sakramenti ya Daraja Takatifu kwa Mashemasi walioandaliwa tayari. Ibada ya Misa ya Upadrisho inatarajiwa kuanza saa 3:30 asubuhi.

Tarehe 28 Aprili 2013, Jumapili ya tano ya Kipindi cha Pasaka, Baba Mtakatifu Francisko ataadhimisha Ibada ya Misa takatifu na kutoa Sakramenti ya Kipaimara. Na kwa kuwaimaarisha Wakristo katika Sakramenti ya Kipaimara ili wawe tayari kutolea ushuhuda wao kwa Kristo na Kanisa lake, Baba Mtakatifu Francisko atakuwa anakunja jamvi la Maadhimisho ya Ibada kwa Mwezi Aprili, 2013.

Mwezi Mei, ambao kadiri ya Mapoke ya Kanisa umetengwa rasmi kwa ajili ya Ibada kwa Bikira Maria, Baba Mtakatifu Francisko atakuwa na majukumu kadhaa ya kutekeleza katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Tarehe 4 Mei 2012, Jumamosi, majira ya saa 12:00 jioni, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuungana na waamini watakaokuwa kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Mkuu lililopo mjini Roma kwa ajili ya kusali Rozari Takatifu, muhtasari wa Injili.

Tarehe 5 Mei 2013, Jumapili ya Sita ya Kipindi cha Pasaka, Baba Mtakatifu Francisko ataungana na mashirika mbali mbali kwa ajili ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kuanzia saa 4:00 asubuhi.

Tarehe 12 Mei 2013, Jumapili ya Saba ya Kipindi cha Pasaka, Baba Mtakatifu Francisko majira ya saa 3:30 asubuhi anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuwatangaza wenyeheri: Antonio Primaldo na wenzake; Laura wa Mtakatifu Katerina wa Siena na Maria Guadalupe Garcìa Zavala kuwa Watakatifu.

Tarehe 18 Mei 2013, Kesha la Pentekoste, Saa 12:00 Jioni, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Baba Mtakatifu Francisko atafanya Kesha la Siku kuu ya Pentekoste, kuzaliwa kwa Kanisa na Siku ya Waamini Walei duniani, wanapotumwa kwenda ulimwenguni kwa ajili ya kuyatakatifuza malimwengu na Vyama vya Kitume.

Tarehe 19 Mei 2013, Siku kuu ya Pentekoste, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, m ajira ya saa 4:00 asubuhi, Baba Mtakatifu ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu pamoja na wanachama wa mashirika na vyama vya kitume. Kwa ufupi, hii ndiyo ratiba elekezi iliyotolewa na Monsinyo Guido Marini, Mshehereshaji mkuu wa Ibada za Kipapa. Kama ilivyo ada, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican, itaendelea kukujuza yale yatakayojiri kutoka katika Ibada hizi. Unaweza pia kufuatilia matukio haya kwa njia ya mtandao wa Radio Vatican kwa anuani ifuatayo:

www.radiovaticana.va







All the contents on this site are copyrighted ©.