2013-04-03 08:09:44

Tume ya haki na amani Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania: tujenge kwa pamoja Tanzania yenye haki na amani!


Mkutano wa kitaifa wa wajumbe wa Tume ya Haki na Amani za majimbo ya Kanisa Katoliki Tanzania na Wanataaluma Wakristo Tanzania (CPT) ulifanyika kwenye Kituo cha Kiroho cha Mbagala tarehe 26-27 Februari, 2013. RealAudioMP3
Wakitafakari na kutaamuli juu ya hali ya maisha nchini na uwajibikaji wa kila mmoja wetu katika kutunza na kujenga haki na amani nchini mwetu, wameonesha kusikitishwa sana na hata kuingiwa hofu na mashaka kwa matukio ya kihalifu na mienendo isiyo ya kawaida inayojidhihirisha nchini nyakati hizi. Waliogopeshwa na kuenea kwa uchoyo na fikra-potofu zinazojidhihirisha kwa misimamo na mihadhara ya kiimani kali na kilokole, ambayo hupotosha ukweli halisi wa dini iliyo na wajibu mkuu wa kulea urafiki na mapatano miongoni mwa watu.
Waliona kuwa ni wajibu wa kila mmoja wetu na wa kila mamlaka ya uongozi wa kijamii na wa kiroho, kujihusisha kwa vitendo thabiti katika ujenzi wa amani na kukubali pasipo shaka yoyote utofauti wetu kuwa ni baraka na chemchemi ya vipaji na rasilimali mbalimbali zitakiwazo katika kila medani za maisha ya taifa na siyo chanzo kisichovumilika cha kukataana na kuhasimiana.
Tunawasihi viongozi wetu wa serikali zote mbili kutoruhusu mashambulio ya aina yoyote kwa watu wa imani mbalimbali, uchomaji wa makanisa, kashfa dhidi ya misahafu na vitabu vitakatifu vya imani tofauti za Watanzania. Tumeona vikundi vya watu mahususi vikiachiwa kuzunguka nchini kote huku vikishambulia waamini wa dini tofauti na ya kwao kwa jeuri bila ya hofu ya sheria wakati Katiba ikizitaka serikali zote mbili na vyombo vya ulinzi kuondoa aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uonevu au upendeleo. Vyombo vya ulinzi sharti vitekeleze wajibu wao na kutoruhusu uwepo wa vikundi hivyo na mienendo ya imani na itikadi kali.
Tunatambua kwamba dini inatumika kwa ajenda ya kisiasa ya kulazimisha dini moja juu ya jamii inayojulikana kufuata dini mbalimbali. Vikundi halifu hivyo vinaikashifu dini wanayoitumia kisiasa kwa madhumuni ya kutwaa utawala wa nchi.
Wakati huu ambao taifa limo katika zoezi la kuandika Katiba mpya, vikundi hivi vidogo vya kichochezi vinaweza kabisa kusambaratisha mchakato huo.
Hali hii inasikitisha sana kwani imesababisha uhai kutoweka kwa mauaji ya wazi wazi ya watu na viongozi wa dini mbalimbali. Wauaji wanatamba kwa jeuri na pasipo woga wa sheria kwa sababu wana watu wao katika ofisi kuu. Tuna sadiki vyombo vya usalama vina uwezo na nyenzo za kuwatia mbaroni wahalifu hao iwapo tu patakuwepo na utashi wa kisiasa.
Tunawasihi watu wote wenye imani; Wakatoliki, Wakristo wa makanisa mengine yote na waumini wa kweli wa Kiislamu, sote kwa pamoja kuonyesha utashi wetu wa kutetea na kudumisha amani tuliyopigania tokea mapambano ya uhuru. Kwa moyo thabiti tukatae kupotoshwa na kikundi cha wachache wanaofadhiliwa na wahalifu bali tusimame imara kujenga Tanzania inayotakiwa na wengi wetu. Madhumuni makuu ya Katiba mpya ni kufikia muafaka wa tutakavyo kuishi kwa umoja kama taifa huru, tukikubaliana katika tofauti zetu za asili na imani pia tukielewana vema na kustahimiliana.
Jambo hilo tunalisisitiza kwa viongozi wetu wa dini, wanaopaswa kutuongoza katika juhudi za kujenga amani na upatanifu, kushutumu kinabii maovu na wapanga maovu ya kuvuruga amani na upatanifu wetu. Viongozi wafafanue viini sababishi vya uvunjifu wa upatanifu wetu ambavyo ni tofauti kubwa za kipato, uwepo wa matajiri wakubwa na masikini wa kutupwa, ukosefu wa ajira kwa vijana na fursa za kazi za kujipatia kipato katika kazi halali za kilimo na ufundi, wakulima wadogo kutokuwa na soko la mazao yao, n.k. Hali hizo ndizo mazalia ambamo chuki hukua na kuwaelekeza vijana pasipo kufikiri kwenye vurugu za kikatili na mauaji ya kinyama.
Tunawaomba viongozi wetu wa dini zote nchini kuteua siku maalumu ambayo watu wote wenye mapenzi mema watadhihirisha utashi wao wa kulinda na kutetea amani ya nchi yetu. Jambo hilo linaweza kutekelezwa kwa namna mbalimbali; kama vile maandamano ya amani, maandamano ya kidini, siku maalumu ya mikutano ya wazi ya sala nchi nzima kama alivyofanya Baba Mtakatifu kule Assisi.
Umuhimu wa maadhimisho ya namna hiyo ni kusema pamoja kwa nguvu na uwazi kwamba Watanzania wanataka amani, upatanifu na umoja katika tofauti zao asili na imani. Kwa miaka mingi tumeishi kwa umoja na tunataka kuendelea kuishi kwa amani iliyo bora kwa ukweli, uhuru, haki na mshikamano kwa maslahi na ustawi wa wote.
Hatutaruhusu kikundi cha wachache wetu kusababisha mageuzi ya kisiasa na kidini kwa malengo yao na kuchukua madaraka na kutawala kidikteta. Historia ya ulimwengu na yanayojiri katika mataifa kadhaa barani Afrika ni fundisho la kutosha na hatutaki Tanzania kuwa mhanga wa mienendo hiyo.
Fikra, maneno na ishara za amani hujenga mawazo na utamaduni wa amani ambao kwao watu huheshimiana, huaminiana katika anga changamfu.
Hilo ndilo ombi letu kwa watu wote wenye mapenzi mema, mtuunge mkono katika jitihada zetu za kujenga haki na amani kwa pamoja.

Dar es Salaam
Februari 27, 2013
Wajumbe wa Mkutano wa Kitaifa wa Tume za Haki na Amani za Majimbo na Wanataaluma Wakristo Tanzania, CPT.
Askofu Mkuu Paul Ruzoka
Jimbo Kuu la Tabora na Mwenyekiti wa Tume ya Haki na Amani, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.