Mshuhudieni Kristo aliyeko mioyoni mwenu kwa uhalisia wa maisha!
Nimemwona Bwana! Ni maneno ya furaha yaliyokuwa yanabubujika kutoka mdomoni mwa Magdalena,
yule mwanamke mdhambi, aliyethubutu kuonesha moyo wa toba kwa machozi yaliyolowanisha
miguu ya Yesu, akaipangusa kwa nywele zake! Ni yule mwanamke aliyekuwa anaangaliwa
kwa "jicho la kengeza" na wale waliokuwa wanajiona kuwa wenye haki, ndiye mwanamke
aliyebahatika pia kupendwa na kusamehewa dhambi zake!
Anakwenda kaburini kumtafuta
Yesu aliyekuwa nanga ya matumaini yake, lakini anaambulia patupu! Moyo wake unagubikwa
na simanzi kuu! Machozi yanamwandaa Magdalena ili kumwona Yesu Kristo Mfufuka! Ni
maneno ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mahubiri yake kwenye Ibada ya Misa Takatifu
aliyoadhimisha katika Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, Jumanne, tarehe 2 Aprili
2013.
Madgalena aliyekutana na kuonana na Kristo Mfufuka anashuhudia kwa furaha
isiyokuwa na kifani. Mwanadamu katika hija ya maisha yake, anapitia vipindi vya furaha,
majonzi na huzuni ya ndani! Je, katika mahangaiko yote haya, anauliza Baba Mtakatifu
Francisko, mwamini ameweza kumwona Yesu Mfufuka akiwa kandoni mwake? Mwamini anapaswa
kusikitika kutoka na dhambi zake na kufurahia pale anapopata nafasi ya kukutana na
Kristo katika hija ya maisha yake.
Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri
yake mafupi kwa waamini waliokuwa wamekusanyika kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae
Marthae, kuomba neema ya kuweza kukutana na Yesu katika undani wa mioyo yao, ili waweze
kuwa tayari kumtolea ushuhuda amini wa uwepo wake endelevu katika hija ya uhalisia
wa maisha yao.