2013-04-02 11:25:47

Vijana wapewa changamoto ya kujiamini katika kushiriki mchakato wa maisha bora zaidi; waachane na matumizi haramu ya dawa za kulevya!


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon, tarehe Mosi Aprili 2013, ametembelea Jumuiya ya Mtakatifu Patrignano, iliyoko Rimini, Italia inayojihusisha na utoaji wa tiba kwa vijana walioathirika kutokana na matumizi haramu ya dawa za kulevya na kuwaomba wahudumu katika Jumuiya hii kuwa na moyo wa huruma na uchungu wanapowahudumia vijana hao wanaofanya hija ya kurekebisha maisha yao, ili kuwa watu wema zaidi.

Jumuiya hii inatoa huduma kwa vijana 1,300 kutoka katika mataifa 28 ambao wamejikuta wakitumbukia katika matumizi haramu ya dawa za kulevya. Katibu mkuu alichukua fursa hii kufungua kinywa pamoja nao na kukumbusha kwamba, hakuna binadamu ambaye ni mkamilifu, kila mtu anaweza kukosea, lakini jambo la msingi kwa vijana hawa kwa sasa ni kuibua karama na vipaji walivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu ili kuvikuza na hatimaye, kuvitumia kwa ajili ya mafao yao na Jamii inayowazunguka. Muda walionao hapo kituoni, iwe ni fursa ya kukomaa na hatimaye, kuachana kabisa na matumizi haramu ya dawa za kulevya kwani zina madhara makubwa kwa binadamu.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema, takwimu za idadi ya watu duniani zinaonesha kwamba, nusu ya vijana wote duniani ni wale walio na umri chini ya miaka ishirini na mitano, wanaosoma na wengine wanafanya kazi mbali mbali ili kuwa na leo na kesho iliyo bora zaidi. Amewataka vijana kuwa na ujasiri na imani kwa ajili ya maisha yao kwa sasa na kwa siku za usoni na kwamba, Jumuiya ya Kimataifa iko bega kwa bega pamoja nao!







All the contents on this site are copyrighted ©.