Papa atembelea Kaburi la Mtakatifu Petro, chini ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro,
mjini Vatican
Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe Mosi Aprili 2013 jioni, ametembelea kwenye
Makaburi yaliyoko chini ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican. Kumbu kumbu
zinaonesha kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anakuwa ni Papa wa kwanza kutembelea makaburi
haya ambayo yamekuwa ni kivutio kikuu kwa wataalam wa mambo ya kale na watalii kutoka
sehemu mbali mbali za dunia kwani huko ndiko kunakosadikiwa kwamba, kuna Kaburi la
Mtakatifu Petro, mwamba wa Kanisa.
Baba Mtakatifu Francisko katika matembezi
yake kwa takribani dakika 45 hatimaye, alifika kwenye Kaburi la Mtakatifu Petro. Baadaye
pembeni kidogo kwenye Kikanisa cha Clemetina hapo alisali kwa kitambo kidogo. Itakumbukwa
kwamba, Kanisa kuu la Mtakatifu Petro limejengwa kwenye kilima ambacho Wakristo wa
Kanisa la mwanzo, walikuwa wanakusanyika ili kusali kwa kificho wakati wa madhulumu
ya Wakristo kwenye utawala wa Kirumi.
Katika matembezi haya, Baba Mtakatifu
Francisko alifuatana na Kardinali Angelo Comastri, mhudumu mkuu wa Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro pamoja na baadhi ya viongozi waandamizi kutoka Vatican. Kwa pamoja walipita
kwenye njia nyembamba zilizokuwa zinatumiwa na Wakristo wakati huo.
Baba Mtakatifu
Francisko amehitimisha matembezi yake ya kiroho kwa kusali kwenye Makaburi ya watangulizi
wake yaliyoko kwenye Pango la Kanisa kuu la Mtakatifu Petro. Hawa ni Papa Benedikto
wa kumi na tano, Pio wa kumi na mbili, Paulo wa sita na Yohane Paulo wa kwanza. Baada
ya kutoka ndani ya Makaburi hayo, Baba Mtakatifu Francisko alisalimiana na baadhi
ya wafanyakazi waliokuwapo katika eneo hili na baadaye alirejea kwenye makazi yake
ya muda huku akifanya mazoezi ya kutembea kwa miguu!
Kunako mwaka 1939 Baba
Mtakatifu Pio wa kumi na mbili aliagiza wataalam wa mambo ya kale kufanya uchunguzi
wa kisayansi kuhusu Mapokeo yaliyokuwa yanaonesha kwamba, chini ya Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro mjini Vatican, kulikuwa na kaburi la Mtakatifu Petro; mahali ambapo Altare kuu
ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro imejengwa juu yake. Uchunguzi wa kisayansi uliofanywa
ndani ya Kanisa hili, uligundua kwamba, kulikuwepo pia Makaburi 22 yaliyokuwa yamesambaa
katika urefu wa mita 70, chini ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro.
Viongozi
wa Kanisa kunako mwaka 1998 wakaamua kufanya ukarabati mkubwa ili kuhifadhi utajiri
huu mkubwa katika ushuhuda wa maisha ya Wakristo wa Kanisa la Mwanzo, kazi ambayo
ilihitimishwa na hatimaye, kufunguliwa Mwezi Mei, 2008.
Baba Mtakatifu Francisko
kwa matembezi haya wakati huu wa Kipindi cha Pasaka ni changamoto ya kuendeleza mchakato
wa Uinjilishaji Mpya katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, kwa kuendeleza
ari na moyo wa Wakristo wa kwanza waliojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza
Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.
Mtakatifu Petro mwamba
wa imani, alisulubiwa miguu juu na kichwa chini, mahali ambapo kunasadikiwa kwamba,
kumejengwa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican