Neema ya Sakramenti ya Ubatizo na Umoja katika Ekaristi Takatifu inawawezesha waamini
kuwa kweli ni vyombo vya huruma ya Mungu
Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu ya Pasaka, wakati waamini wengi wakiwa bado wanasherehekea
Siku kuu ya Pasaka, kwa mara nyingine tena aliungana na waamini waliofurika kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ili kusali pamoja Sala ya Malkia wa Mbingu
inayotumika katika Kipindi cha Pasaka. Katika tafakari yake Baba Mtakatifu Francisko
anasema kwamba, Pasaka ni kiini cha Imani ya Kanisa na kwamba, nguvu ya Kristo Mfufuka
iwafikie watu wote wanaoteseka; wale ambao wanahitaji kuimarishwa katika imani na
matumaini.
Baba Mtakatifu anasema, Kristo ameshinda uovu kwa daima, ni changamoto
na mwaliko kwa waamini wa kila nyakati kuupokea ujumbe na kuumwilisha katika uhalisia
wa maisha katika historia na Jamii inayowazunguka. Anawaalika kwa namna ya pekee Wakristo
waliobatizwa katika: Kesha na Siku kuu ya Pasaka kwa Mwaka huu kushuhudia imani waliyoipokea
kutokana na Sakramenti za Kanisa.
Kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, watu wanafanyika
kuwa ni watoto wateule wa Mungu; Ekaristi takatifu inawaunganisha na Kristo kwa njia
ya uhalisia wa maisha yake: kwa maneno, lakini zaidi kwa njia ya matendo yao. Neema
inayobubujika kutoka katika Sakramenti za Pasaka ina nguvu ya kumkirimia mwamini mabadiliko
ya ndani kama mtu binafsi, familia na katika mahusiano ya kijamii.
Yote haya
yanatendeka kwa njia ya moyo wa mwanadamu, ambao uko tayari kupokea neema kutoka kwa
Kristo Mfufuka ili kubadilika na kuwa mtu mwema zaidi kwa kutambua kwamba, ubaya unaweza
kumtenda mtu mwenyewe pamoja na jirani zake. Ni mwaliko wa kuhakikisha kuwa nguvu
na ushindi wa Kristo mfufuka unabaki na kutenda kazi ndani ya wafuasi wake na hivyo
kuenea na kuwasaidia watu wengine zaidi. Bila neema ya Mungu, hakuna jambo linalowezekana.
Baba
Mtakatifu Francisko anasema kwamba, kwa njia ya neema ya Sakramenti ya Ubatizo na
Umoja katika Fumbo la Ekaristi Takatifu, waamini wanaweza kuwa kweli ni vyombo vya
huruma ya Mungu. Waamini wanakabiliwa na utume ambao unawasukuma kuhakikisha kwamba,
wanamwilisha Sakramenti za Kanisa katika uhalisia wa maisha yao. Waamini wafurahie
fursa ya kuwa ni vyombo vya neema ya Kristo, kama matawi yanayosimikwa katika Kristo
ambaye kimsingi ndiye shina lenyewe, linalorutubisha na Roho Mtakatifu.
Baba
Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kusali kwa njia ya jina la Yesu, aliyeteswa,
akafa na kufufuka kutoka katika wafu, ili kwa njia ya maombezi ya Bikira Maria Fumbo
la Pasaka liweze kutenda kazi ndani yao, kwa nyakati hizi, ili chuki na uhasama vitoe
nafasi kwa upendo; uongo utoweke na ukweli uweze kutawala; kisasi kiache nafasi kwa
fadhila ya msamaha; huzuni igeuke kuwa furaha.
mara baada ya kutafakari na
kusali kwa pamoja Sala ya Malkia wa Mbingu, kwa mara nyingine tena Baba Mtakatifu
Francisko, amewasalim na kuwatakia kila la kheri na baraka wakati huu Kanisa linapotangaza
kwa nguvu Kristo amefufuka. Pasaka Njema.