Tunahesabiwa haki kwa njia ya imani katika Damu Azizi ya Yesu Kristo!
Padre Raniero Cantalamessa, katika mahubiri yake kwa Maadhimisho ya Ijumaa Kuu, tarehe
29 Machi 2013, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Kanisa linapofanya
kumbu kumbu ya Mateso na Kifo cha Kristo, Ibada ambayo imehudhuriwa na Baba Mtakatifu
Francisko, amekazia kwa namna ya pekee kwamba, waamini wanahesabiwa haki kwa njia
ya imani katika Damu Azizi ya Yesu Kristo.
Mada hii inakwenda sanjari na
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani ambayo inaokoa na kuushinda ulimwengu, pale Mwenyezi
Mungu anaponyoosha mkono wa neema na baraka kwa mwanadamu, kiasi cha kuanzisha agano
jipya na la milele.
Hapa waamini wanachangamotishwa kufungua malango ya mioyo
yao ili kumwamini Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu kwa ajili
ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti, ili hatimaye, kumhesabia
haki mwanadamu. Yesu Kristo ni chemchemi ya maisha mapya. Ibada hii pia ni mwanzo
mpya wa utume wa Baba Mtakatifu Francisko kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, changamoto
na mwaliko wa kumtambua na kuthamini uwepo wa Kristo katika hija ya maisha ya kila
mwamini.
Waamini watambue dhambi na mapungufu yao, wawe tayari kuyakiri kama
alivyofanya yule mtoza ushuru aliyerudi nyumbani akiwa amehesabiwa haki, akiwa anatembea
katika utu mpya. wakishahesabiwa haki itokayo katika imani, waamini wawe na amani
kwa Mungu, kwani kwa njia ya Yesu Kristo wanaweza kufurahia na kutumainia utukufu
wa Mungu, wakijua kwamba, dhiki kazi yake ni kuleta saburi na kazi ya saburi ni uthabiti
wa moyo na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini na tumaini halitahayarishi; kwa maana
pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yao kwa njia ya Roho Mtakatifu waliyempokea.
Kwa
njia ya kifo na ufufuko wa Yesu Kristo anasema Padre Cantalamessa, dunia imefikia
hitimisho lake, kwani Yesu Kristo amepaa kurudi kwa Baba yake wa mbinguni na anakaa
kuumeni kwake. Hapa ni mwanzo wa mbingu na dunia mpya, licha ya uwepo wa taabu, magumu
na hata kifo, lakini haya ni mambo ambayo Yesu ameyashinda na ni Bwana wa yote. Yesu
ameshinda kifo na kifo hakina nguvu tena. Imani ya Kikristo liwe ni jibu makini katika
changamoto na kinzani mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu mamboleo.
Msalaba wa Kristo uwe ni kiungo makini miongoni mwa waamini katika mchakato
wa Uinjilishaji Mpya, kwa kuwatangazia watu Habari Njema ya Wokovu kwamba, Yesu amewakomboa
kutoka katika utumwa wa dhambi na mauti. Kwa njia ya mateso na kifo chake, Yesu anawatuma
wafuasi wake kuwatangazia wote Habari Njema ya Wokovu, ili waweze kuyainua macho yao
wapate kumtaza yule waliyemchoma ubavuni kwa mkuki!
Ni changamoto kwa waamini
kutangaza habari ya faraja na wokovu unaobubujika kutoka kwa Kristo. Uinjilishaji
ni zawadi ya Msalaba wa Kristo, unaodhihirisha Moyo wake Mtakatifu uliotobolewa humo
ikatoka damu na maji, kielelezo cha upendo wa hali ya juu kutoka katika Fumbo la Utatu
Mtakatifu. Huu ni mwaliko wa kutangazia watu huruma na upendo wa Mungu, wakitambua
kwamba, Uinjilishaji kwa hakika ni zawadi ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, inayopania
kujenga na kuimarisha Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa.
Msalaba wa Kristo
umevunjilia mbali utengano uliokuwapo kati ya waamini wa Makanisa mbali mbali, urasimu,
ibada, sheria na kanuni zilizopitwa na wakati. Hii ni changamoto kwa Mama Kanisa kutoka
na kuwaendea wale walioko pembezoni mwa jamii, wanaokabiliwa na uwepo wa dhambi, magumu,
ukosefu wa haki msingi za binadamu, ujinga, umaskini, maradhi, kinzani za kidini na
madhulumu mbali mbali.
Hiki ni kipindi cha kusoma alama za nyakati, tayari
kuibua mikakati ya kichungaji, inayopania kujenga na kuimarisha Kanisa la Kristo,
kwa kutambua kwamba, Roho Mtakatifu anawasaidia kutekeleza wajibu huu msingi kwa ajili
ya utume na maisha ya Kanisa. Kuna matumaini makubwa kwa Kanisa kuanza kipindi kipya
cha maisha na utume wake; kipindi ambacho kina sheheni matumaini na watu wako tayari
kuyapokea matumaini haya anasema Padre Raniero Cantalamessa, hata kwa gharama ya maisha!