2013-03-30 07:12:59

Ibada ya Ijumaa kuu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican


Mama Kanisa katika adhimisho la Ijumaa kuu anafanya kumbu kumbu ya mateso na kifo cha Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Siku ya kufunga kama kielelezo cha nje kinachoonesha ushiriki wa waamini katika mateso ya Yesu Kristo. Hakuna adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu kwani Kristo ambaye ndiye chemchemi ya Sakramenti zote za Kanisa anateseka na hatimaye, kufa Msalabani.

Ijumaa kuu jioni, Kanisa limeadhimisha Mateso na Kifo cha Yesu, anayejionesha kuwa ndiye Mtumishi wa Mungu aliyetabiriwa na Manabii katika Agano la Kale. Ni Mwana Kondoo wa Mungu anaye yamimina maisha yake kwa ajili ya ukombozi wa wengi.

Msalaba ni alama kuu inayochukua kipaumbele cha pekee katika Maadhimisho ya Ijumaa Kuu. Ni kielelezo cha Mti wa Ushindi wa Kristo dhidi ya dhambi na mauti, ndiyo maana, waamini wamepata fursa ya kuweza kuabudu Msalaba wa Kristo.

Mjini Vatican, Ibada ya Ijumaa kuu ambayo kimsingi imegawanyika katika sehemu kuu tatu yaani: Liturujia ya Neno la Mungu inayohusisha mahubiri ambayo kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican yametolewa na Padre Raniero Cantalamessa, Mhubiri wa nyumba ya Kipapa pamoja na Sala za Waamini kwa ajili ya Kanisa na Ulimwengu katika ujumla wake. Sehemu ya Pili ni Liturujia ya Ibada ya Kuabudu Msalaba na Sehemu ya tatu ni Ibada ya Komunio Takatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.