Tafakari ya kina kuhusu Kesha la Jumamosi Kuu: Usiku Mtakatifu
Ninakuleteeni furaha ya Pasaka kwa njia ya tafakari ya Neno la Mungu. Kesha la Pasaka
yaani Jumamosi kuu ni usiku mtakatifu ambapo Kristo mshindi amejipatia taji kwa kuyashinda
mauti.
Ni siku ambayo
Kristo hayumo tena kaburini bali yu mzima na kwa maana hiyo Kanisa popote duniani
linashangilia na kuimba aleluya. Katika Liturujia ya usiku mtakatifu Kanisa laelezea
jinsi ambavyo Kristo ni Nuru, linaimba sifa za nuru hii kwa njia ya Mbiu ya Pasaka.
Kanisa linashangilia ushindi toka upotevu wa mwanadamu na kuelekea uhuru kamili unaoletwa
na Kristo mfufuka.
Liturujia ya Jumamosi Kuu imegawanyika katika sehemu kuu
nne, yaani: Liturujia ya Mwanga; Liturujia ya Neno, Liturujia ya ubatizo na Liturujia
ya Ekaristi Takatifu. Katika sehemu hizi kuu nne Mama Kanisa ataka tuelewe polepole
jinsi ukombozi ulivyotufikia kwa njia ya Masiha, aliyeteswa, akafa na kufufuka siku
ya tatu.
Katika Litrujia ya Mwanga kawaida tunaanza na ishara ya moto ambao
huleta joto na mwanga, hufukuza baridi na giza. Moto unaowaka huonesha uwepo wa Mungu
katikati yetu. Alama hii tunaiona pale Wana wa Israeli walipokuwa wakitoka Misri waliongozwa
na moto katika wingu. Katika Agano jipya tunaona ndimi na miali ya moto siku ya Pentekoste
na hivi Roho Mtakatifu alitua kwa kila mmoja wa Mitume waliokuwa pamoja na Bikira
Maria.
Moto ni alama ya utakaso toka uovu na kuelekea utakatifu au wajibu wa
kitume, hebu kumbukeni jinsi Nabii Isaya alivyowekewa kaa la moto kinywani mwake na
hivi akatangaziwa utakaso wa roho tayari kwa kazi ya kinabii. Isa. 6:6-7.
Katika
Liturujia ya Kanisa kwa sasa, moto ubarikiwa ili uwe ishara ya upendo na maelewano
katika familia, ishara ya kufukuza giza yaani shetani katika maisha ya kikristu. Kumbe
tunapowasha Mshumaa wa Pasaka na mishumaa yetu mingine toka moto huu tunataka kumwahidi
Bwana zawadi nzuri ya upendo, utayari, heshima tutakayomrudishia sisi wenyewe. Kwa
ujumla mshumaa ni uwepo wa Mungu katikati ya mataifa, katikati yetu na tunasema ni
Mungu milele. Angalia taa ya milele kanisani ashilio la uwepo wa Mungu katika Ekaristi
Takatifu daima katikati yetu.
Maandamano toka Moto wa Pasaka hadi kuimbwa Mbiu
ya Pasaka SIFA KWA MSHUMAA ishara ya Kristo humaanisha kuwa kanisa linatoa sifa kwa
Mwanga mtakatifu ndiye Kristo mfufuka. Mshumaa wa Pasaka katika Litrujia ya ubatizo
utatumbukizwa mara tatu, iliyo ishara ya Utatu Mtakatifu kwa maana ya kuyaweka wakfu
maji katika Utatu Mtakatifu na kwa njia hiyo mwovu hufukuzwa ili watakaobatizwa katika
kisima hicho wapate nguvu ya Utatu Mtakatifu.
Mpendwa mwanapasaka, baada ya
litrujia ya mwanga huanza litrujia ya Neno la Mungu ambamo kanisa hutafakari historia
ya mwanadamu tangu kuumbwa kwake hadi anapokuja mkombozi na kumalizia na ufufuko kilele
cha mapendo ya Mungu kwa mwanadamu. Katika somo la kwanza tunaona Mungu anaumba kila
kitu na anaona ni chema kabisa. Kisha mama kanisa anatuwekea mbele yetu Ibrahimu baba
wa imani katika somo la pili. Matunda ya imani ya Ibrahimu ni uzao, baraka tele na
wokovu. Mwaliko kwetu ni kumsifu Mungu kwa kutuumba na kuomba kujaliwa imani kama
ya Ibrahimu.
Katika somo la tatu toka kitabu cha kutoka tunapata kugundua
maongozi ya Mungu na upendo wake kwa wanadamu. Anawatoa Misri na anawavusha bahari
na mto ishara ya ubatizo, yaani kuzamishwa na kuibuka kuelekea ng’ambo ya pili ulioushindi
na utakatifu. Katika somo la Waraka kwa Warumi ujumbe wa mahsusi ni kuwa kuishi kwetu
ni Kristo, kwa maana tulikufa naye katika mauti na kufufuka naye katika ubatizo. Sasa
tuko wapya na hivi mwaliko ni kuacha dhambi na kuendelea na maisha mapya.
Katika
somo la Injili Habari ya ufufuko na ushindi dhidi ya mauti ndiyo imetanda na kupamba
kila aina ya adhimisho la pasaka. Tunaona akina mama ambao Bwana ameamua kuwatuza
wao kwanza zawadi ya ufufuko ikiwa pia ni ishara ya kuinuliwa kwao toka ukiritimba
wa kiyahudi. Wanaenda kaburini alfajiri na mapema. Wakiwa na mashaka juu ya nani atawaondolea
jiwe juu ya kaburi, wanakuta jiwe halipo! Jiwe ni alama ya kandamizo na hivi kutokuwepo
ni kwamba, Bwana ni mshindi amelitupilia mbali.
Wanamwona kijana mwenye mavazi
meupe na anawapa taarifa kuwa Bwana hayupo amefufuka kumbe waende wakaseme kwa wanafunzi
wake kuwa awatangulia Galilaya kama alivyokuwa amewaambia. Kijana mwenye vazi jeupe
ni alama ya malaika anayetangaza kuwa Kristo ni wa juu na hivi ni mtakatifu na mzima.
Taarifa ya kwamba nendeni Galilaya ina maana kubwa sana ya kwamba wasibaki
alipofia bali wafikirie ufufuko na wakaende kwenye jumuiya ya watu si kaburini. Ni
mwanzo wa umisionari, ni mwanzo wa msingi wa maisha ya mapendo ya kichungaji kwa jumuiya
ya watu.
Neno la Mungu ni taa ya kutuongoza na daima kama tangazo la imani
huita na kuzaa matunda ndiyo ubatizo. Kumbe, baada ya litrujia ya Neno hufuata litrujia
ya ubatizo ambamo mama kanisa hupata watoto wapya. Kisima cha ubatizo hubarikiwa kwa
mshumaa wa pasaka na hivi nguvu ya Utatu Mtakatifu kwa ajili ya wabatizwa huwekwa
na Kristo mwenyewe aliye nuru na mwanga kwa wote. Kisima cha ubatizo hugeuka kuwa
tumbo la uzazi kama mama, huzaa watoto taifa teule la kikuhani, kifalme na kinabii.
Kwa njia ya ubatizo mtu huifia dhambi na kuacha mambo ya kale na kuingia maisha mapya.
Ubatizo ni kielelezo msingi na hasa ndiyo ufufuko. Wale waliokwisha batizwa
zamani wanaalikwa katika litrujia ya ubatizo kurudia ahadi zao za ubatizo na kusonga
mbele katika ufufuko. Na kwa jinsi hiyo kanisa linakua.
Mwishoni, mama kanisa
huadhimisha litrujia ya Ekaristi Takatifu ambamo sasa waamini wapya hushirikishwa
kwanza ukamilifu wa sakramenti za kuingizwa katika ukristu. Hushiriki meza ya mapendo
ya Kristu kwa mwanadamu. Hujipatia uzima wa milele kama tufahamuvyo toka injili ya
kuwa aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu ataishi milele.
Waamini wote
hushiriki matunda ya pasaka Ekaristi Takatifu. Ni sadaka ya Kristo msalabani iliyo
hai katika ufufuko. Ekaristi ni umoja na chimbuko la umoja wa kanisa na hivi wote
waliofamilia moja wanashiriki mkate mmoja wa mbinguni.
Mpendwa, nikutakieni
heri na baraka tele za Mungu katika sherehe za Pasaka ukakirimiwe yote mema sasa na
daima na milele. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard
Tiganya, C.PP.S.