Msimruhusu mtu yeyote yule kuwapokonya tena matumaini yenu!
Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Maadhimisho ya Karamu ya Mwisho kwenye Gereza
la Watoto la "Casal del Marmo", amemshukuru Mama Paola Severino Waziri wa Mambo ya
ndani wa Italia kwa niaba ya Serikali ya Italia. Kwa namna ya pekee, amewashukuru
vijana waliohudhuria Ibada ya Misa Takatifu kwa kusema kwamba, amepata furaha kubwa
sana moyoni mwake kwa kuweza kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu pamoja nao!
Kwa
namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko amewatia shime vijana hawa kusonga mbele
kwa imani na matumaini mapya na kamwe wasitoe nafasi kwa mtu yoyote kuwapokonya matumaini
walio nayo moyoni! Matumaini haya yawasaidie kusonga mbele kwa kujiamini zaidi.
Kijana
mmoja mwenye ujasiri, amemuuliza Baba Mtakatifu Francisko, kwa nini ameamua kwenda
kuwatembelea? Baba Mtakatifu amemjibu kijana huyu kwa kusema kwamba, alijisikia kutoka
katika undani wa moyo wake kuja kuwatembelea na kuwafariji, kielelezo cha fadhila
ya unyenyekevu na huduma inayopaswa kuoneshwa na Askofu.
Baba Mtakatifu anasema,
wakati mwingine mambo ya maisha ya kiroho hayana maelezo ya kina, kwani huu ni msukumo
kutoka katika undani wa mtu mwenyewe. Baba Mtakatifu Francisko amewaomba vijana hawa
ambao wanatumikia adhabu zao gerezani humo, kumwombea katika maisha na utume wake.
Waziri
wa Mambo ya ndani wa Italia, akihojiwa na Radio Vatican anabainaisha kwamba, maneno
ya Baba Mtakatifu Francisko yamewagusa vijana hawa na kuacha chapa ya kudumu. Vijana
wameonesha jicho la upendo wakati wote wa maadhimisho wa Karamu ya Mwisho ambayo Baba
Mtakatifu ameamua kuiadhimisha kwenye Gereza la Watoto watukutu!
Amewaonjesha
matumaini na kuwachangamotisha wahudumu wa magereza kuonesha upendo na moyo wa huduma
kwa wafungwa waliomo gerezani. Hii ndiyo hali iliyojionesha pia katika macho ya Askari
Magereza, Wafanyakazi, Wahudumu na watu wanaojitolea Gerezani hapo.
Huu ndio
ujumbe unaotolewa na Baba Mtakatifu Francisko si tu kwa ajili ya Magereza ya Italia,
bali Magereza yawe ni shule inayosaidia mchakato wa kuleta mabadiliko katika maisha
ya mtu, ili baada ya kutumikia adhabu yake gerezani arudi na kujiunga tena na Jamii
akiwa ni mtu mwema. Magereza yasiwe ni mahali pa mateso na mahangaiko ya watu! Utu
na heshima ya wafungwa viheshimiwe na kuthaminiwa, licha ya makosa yao, bado wanaendelea
kuwa ni watu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.