2013-03-29 09:29:55

Ekaristi Takatifu na Daraja Takatifu ni Sakramenti Pacha!


Kardinali John Njue, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Nairobi, Kenya, Alhamisi kuu, asubuhi, ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kubariki Mafuta Matakatifu, kwenye Kanisa kuu la Familia Takatifu, lililoko Jijini Nairobi. Kardinali Njue amewakumbusha Mapadre kwamba, Upadre ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Kanisa lake. Mapadre ni viongozi waliodhaminishwa utume wa kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa, ambayo wanapaswa kuwashirikisha waamini wao.

Kardinali Njue anasema kwamba, Sakramenti ya Daraja Takatifu na Ekaristi Takatifu ni Sakramenti Pacha, kwani huwezi kuadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu bila ya kuwa na Padre na huwezi kupata Daraja Takatifu nje ya Sakramenti ya Maadhimisho ya Ekaristi Takatifu.

Mapadre katika ulimwengu mamboleo wanaendelea kukabiliana na changamoto mbali mbali katika maisha na utume wao, jambo la msingi ni kuishi ile fadhila ya unyenyekevu pamoja na kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na Jirani. Mapadre ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa, wanapaswa kukoleza na kung'ara kwa njia ya utakatifu wa maisha yao.

Mapadre wawasaidie waamini kuifahamu imani, kuiadhimisha, kuimwilisha na kuisali, kama ushuhuda wa imani tendaji katika hija ya maisha ya waamini hapa duniani. Mapadre wanayo dhamana kubwa katika mchakato mzima wa Uinjilishaji Mpya, ili kuwasaidia waamini kuweza kuyatakatifuza malimwengu, ili hatimaye, dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Katika Maadhimisho ya Misa ya Krisma ya Wokovu, Mapadre wa Jimbo kuu la Nairobi, wamerudia ahadi zao za utii kwa Kardinali John Njue, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Nairobi.







All the contents on this site are copyrighted ©.