Njia ya Msalaba, ni kilio dhidi ya ukosefu wa haki msingi za binadamu, changamoto
ya kukumbatia: amani, majadiliano, upendo na mshikamano wa dhati
Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Ijumaa kuu, Mama Kanisa anapofanya
kumbu kumbu ya mateso na kifo cha Kristo Msalabani, anatarajiwa kuongoza Ibada ya
Njia ya Msalaba kwenye Magofu ya Coloseo yaliyoko mjini Vatican.
Tafakari ya
Njia ya Msalaba yenye vituo kumi na vinne kadiri ya Mapokeo, imetolewa na Kardinali
Bèchara Boutros Rai, Patriaki wa Kanisa la Kimaroniti, kwa ombi maalum kutoka kwa
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita.
Katika mahojiano maalum na
Gazeti la L’Osservatore Romano, Patriaki Boutros Rai anabainisha kwamba, mawazo makubwa
yaliyojitokeza katika tafakari ya Njia ya Msalaba kwa Ijumaa kuu ni mwaliko na changamoto
ya kugundua kwa mara nyingine tena fadhila ya amani, mshikamano wa upendo kwa wote
wanaoteseka sehemu mbali mbali za dunia kutokana na ukosefu wa haki msingi za binadamu.
Hii ni tafakari iliyoandikwa na vijana kutoka Lebanoni wakiongozwa na Kardinali Boutros
Rai.
Hawa ni vijana walioguswa na cheche za mtutu wa bunduki na kwamba, kifo
daima kiko mbele ya macho yao. Wanaendelea kushuhudia mateso ya wananchi wa Syria
na nchi jirani, ambako raia wanalazimika kuyakimbia makazi yao kutokana na vita na
hivyo kujikuta wakiwa wageni hata katika nchi yao wenyewe.
Ni watu wanaokabiliana
na mateso, lakini bado wana matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi, baada ya kufanya
tafakari ya kina kuhusu mateso, kifo na ufufuko wa Kristo katika hija ya maisha yao
kama Wakristo. Mateso kwa njia ya Kristo yanapata maana mpya, kwani haya ni kwa ajili
ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Vijana wanasema, wote
wanaoteseka wanaweza kuonja tena matumaini katika maisha yao kwa njia ya ufufuko wa
Yesu Kristo kutoka katika wafu.
Patriaki Boutros Rai anabainisha kwamba, wazo
la kuwapatia vijana wa Lebanon dhamana ya kuandika tafakari ya Njia ya Msalaba kwa
Mwaka 2013 kutoka kwa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, ni kitendo
cha kinabii kabisa. Papa Benedikto wa kumi na sita, aliwataka vijana kuonesha magumu
na machungu wanayokabiliana nayo; matumaini na matarajio ya wananchi wanaoishi huko
Mashariki ya Kati.
Ni tafakari zinazopata chimbuko lake katika Maandiko Matakatifu;
mateso na mahangaiko ya wananchi walioko Mashariki ya Kati na Ulimwengu kwa Ujumla
na mwishoni ni matumaini yao kwa Kristo. Hizi ni tafakari ambazo zimeandaliwa na Vijana
katika makundi na Patriaki Boutros Rai, akahitimisha kazi hii kubwa kwa kuhariri yale
ambayo vijana walikuwa wameyatafakari katika hija ya maisha yao ya kila siku.
Njia
ya Msalaba ni fursa makini kwa kila mwamini na wote wenye mapenzi mema kuweza kukutana
na Kristo katika mateso yake kama binadamu. Kila kituo cha Njia ya Msalaba ni Mlango
maalum wa kukutana na Yesu katika safari yake kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka
katika lindi la dhambi na mauti.
Uso wa Yesu Mteswa unaendelea kujionesha
sehemu mbali mbali za dunia, changamoto na mwaliko kwa kila mwamini kuubeba vyema
Msalaba wake kisha kumfuata Kristo, akijitahidi kugundua maana ya Mateso yanayokomboa.
Lengo ni kutowakatisha tamaa wale wanaomfuasa Kristo, bali kila mwamini ajitahidi
kukamilisha ndani mwake yale mateso yanayopungua kutoka kwa Kristo kwa ajili ya Kanisa
lake.
Ni tafakari zinazogusa mahangaiko ya watu kutokana na vita, kinzani na
migogoro ya kijamii; uvunjifu wa haki msingi za binadamu na ukosefu wa amani na usalama.
Hadi sasa Jumuiya ya Kimataifa imeshindwa kutoa suluhu ya kudumu kutokana na mgogoro
wa kivita unaoendelea huko Mashariki ya Kati. Yote haya ni matokeo ya misimamo mikali
ya kiimani. Vijana wa Lebanon wameyaona na kuyafanyia tafakari ya kina.
Katika
tafakari hii makini, Vijana wa Lebanon wameongozwa kwa namna ya pekee na Waraka wa
Kichungaji wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Kanisa Mashariki ya Kati au
kama unavyojulikana kwa Lugha ya Kilatini “ Ecclesia in Medio Oriente”.
Hapa mkazo unawekwa zaidi kwenye umoja na mshikamano; majadiliano ya kidini na kiekumene
na kwamba, kama waamini Imani inapaswa kupewa msukumo wa pekee katika maisha yao kama
yalivyo pia matumaini.
Baada ya mateso na kifo, kuna ufufuko wa Kristo kutoka
katika wafu! Hii inaonesha kwamba, kimsingi Ijumaa kuu haina maana sana, ikiwa kama
Yesu Kristo hasingelifufuka kutoka katika wafu. Ufufuko wa Kristo ni ushindi dhidi
ya dhambi na mauti.
Baba Mtakatifu Francisko anashiriki kwa mara ya kwanza
katika Njia ya Msalaba kuzunguka Magofu ya Colosseo kwa mara ya kwanza kama Khalifa
wa Mtakatifu Petro. Hawa ni viongozi wa Kanisa ambao wameguswa kwa namna ya pekee
na mateso pamoja na mahangaiko ya wananchi wanaoishi Mashariki ya Kati. Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita, wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Lebanon kuanzia
tarehe 14 hadi 16 Septemba 2012 alibahatika kukutana na kuzungumza na viongozi wa
Kikristo na Kiislam, akakazia umuhimu wa kujenga na kudumisha majadiliano ya kidini
na kiekumene kama njia ya kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na upatanisho
wa kweli.
Ni matumaini ya wananchi wa Mashariki ya Kati kwamba, Baba Mtakatifu
Francisko ataendeleza mchakato wa Kanisa kutafuta na kukoleza misingi ya haki, amani,
upendo, mshikamano na upatanisho. Papa Francisko tangu alipochaguliwa, alifafanua
maana ya jina lake na hadi sasa ameonesha ule utashi wa kutaka kuwa karibu na kwa
ajili ya watu.