2013-03-28 10:52:22

Jumapili ya huruma ya Mungu, Papa Francisko kuadhimisha Ibada kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano


Katika maadhimisho ya Jumapili ya Huruma ya Mungu, hapo tarehe 7 Aprili 2013, Siku kuu iliyoanzishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili kunako mwaka 2000, Baba Mtakatifu Francisko ataadhimisha rasmi Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, ambalo ni Makao Makuu ya Jimbo kuu la Roma. Ibada hii itafanyika majira ya saa 11:30 Jioni kwa Saa za Ulaya.

Baba Mtakatifu Francisko katika Katekesi yake ya kwanza kwa waamini, mahujaji na wageni iliyofanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, aliwaomba waamini kwa namna ya pekee, kumwombea, kwani anatambua kwamba, hata Yeye ni Mdhambi, lakini anatumainia huruma ya Mungu.

Ibada ya huruma ya Mungu ilianzishwa na kuendelezwa na Mtakatifu Faustina, ikawa ni changamoto kwa waamini wote kuwa kweli ni mashahidi wa huruma ya Mungu katika hija ya maisha yao hapa duniani. Itakumbukwa kwamba, Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, alifariki dunia jioni iliyotangulia Maadhimisho ya Jumapili ya Huruma ya Mungu, kunako mwaka 2005.







All the contents on this site are copyrighted ©.