2013-03-27 09:48:30

"Msigeuze mgogoro wa kisiasa kuchukua sura ya kidini kwani ni hatari kubwa"


Askofu mkuu Diudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Afrika ya Kati akihojiwa na Radio Ufaransa amebainisha kwamba, wananchi wanakabiliwa na hali ngumu na wasi wasi wa maisha baada ya waasi wa kikundi cha Seleka kuuteka mji mkuu wa Bangui na baadaye kutangaza kusitishwa kwa matumizi ya Katiba na kwamba, Bunge halina nguvu tena.

Kumekuwepo na vitendo vya uporaji wa mali na mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, jambo ambalo Askofu mkuu Nzapalainga anasema, linamsikitisha sana. Anawaomba vikosi vya waasi kulinda raia na mali zao na kuwajibika kikamilifu kwa vitendo vyote wanavyoendelea kufanya nchini humo. Jumapili iliyopita, watu wengi waliporwa mali zao. Askofu mkuu ameonya kwamba, mgogoro wa kisiasa usigeuzwe kuwa ni chanzo cha choko choko za kidini nchini humo. Viongozi wa Vikosi vya waasi waliofanya mapinduzi wanapaswa kukomesha vitendo vya uporaji wa mali ya wananchi na kuwafikisha wahusika kwenye mkondo wa sheria.

Kwa namna ya pekee, Askofu mkuu Nzapalainga amewataka wananchi kujiepusha na chokochoko zinazoweza kupelekea kinzani na hatimaye vita vya kidini nchini humo. Viongozi wa kidini waheshimiwe na kupatiwa ulinzi, kama ambavyo pia wananchi wanapaswa kulindwa dhidi ya vitendo vinavyoweza kusababisha maafa makubwa.









All the contents on this site are copyrighted ©.