2013-03-27 08:12:18

Jipangeni sawa sawa kwa ajili ya mchakato wa uchaguzi mkuu Zimbabwe!


Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe linawataka wananchi wa Zimbabwe kujiandaa kikamilifu kushiriki katika mchakato wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu, kwani hili litakuwa ni tukio muhimu sana katika maisha yao, kama ilivyokuwa kunako mwaka 1980 walipojipatia uhuru wao kutoka kwa Mwingereza, wakapandisha bendera yao wenyewe na kuanza kutembea kifua mbele kama watu huru!

Maaskofu wanasema, umefika wakati wa kuachana na siasa za chuki na uhasama; uvunjifu wa misingi ya haki na amani; vitisho na ubabe; ukosefu wa misingi ya ukweli na uwazi; uwajibikaji; rushwa na ufisadi na badala yake, wananchi wa Zimbabwe sasa wanapaswa kufungua milango yao ili kuonesha ukomavu wa kisiasa na kidemokrasia.

Hivi ndivyo wanavyoandika Maaskofu Katoliki Zimbabwe katika barua yao ya kichungaji, wakati huu wanapojiandaa kwa ajili ya mchakato wa uchaguzi mkuu baada ya kupitisha kwa kura nyingi Muswada wa Katiba Mpya ya Zimbabwe kwa kupiga kura ya maoni.

Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe linasema kwamba, wananchi wengi wa Zimbabwe wanatumaini kwamba, uchaguzi mkuu wa Mwaka 2013, utakuwa huru na wa haki na hivyo kuifanya Zimbabwe kuonekana tena katika ramani ya kimataifa, baada ya kupitisha Katiba Mpya na kufanya mabadiliko makubwa katika medani mbali mbali za maisha ya watu!

Tarehe 16 Machi 2013, Zimbabwe ilipitisha Katiba Mpya iliyoungwa mkono na Rais Robert Mugabe pamoja na Waziri Mkuu Morgan Tsvangirai, ambao kwa miaka mingi wamekuwa ni maadui kisiasa, waliolazimika kunako mwaka 2008 kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa.

Katiba Mpya ya Zimbabwe ina mabadiliko makubwa yanayolenga kudhibiti madaraka ya Rais pamoja na kutetea haki msingi za binadamu. Matamko ya Rais, yatapaswa kuungwa mkono na wabunge wengi katika vikao vya Bunge. Mabadiliko makubwa yanatarajiwa kuanza kutekelezwa mara baada ya kukamilika kwa mchakato wa uchaguzi mkuu nchini Zimbabwe.

Maaskofu wanasema kwamba, uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2013 ni fursa nyingine muhimu kwa wananchi wa Zimbabwe kuonesha ukomavu na uvumilivu wa kisiasa, wakitambua machafuko yaliyoibuka nchini humo na kupelekea maelfu ya watu kuyakimbia makazi yao na Zimbabwe iliyokuwa imecharuka kwa maendeleo Barani Afrika, ikajikuta ikisua sua kwa kuandamwa na kinzani pamoja na migogoro ya ndani. Matokeo yake yalikuwa ni kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Miaka kumi iliyopita, wananchi wengi wa Zimbabwe wamejikita wakielemewa zaidi na masuala ya kisiasa.

Umefika wakati kwa wananchi wa Zimbabwe kuondokana na utawala mgando, rushwa na ufisadi; tatizo la watu kuyakimbia makazi yao; sera na siasa za chuki na uhasama; ukabila na udini. Kanisa Katoliki kwa upande wake, limeendelea kuwajengea wananchi uwezo wa kujenga na kuimarisha utamaduni wa amani, haki na upatanisho, kama sehemu ya mchakato unaopania kuponya madonda ya chuki, kinzani na migogoro ya kijamii iliyojitokeza miongoni mwa wananchi wa Zimbabwe.

Lengo ni kuendelea kuimarisha haki, msamaha na upatanisho wa kitaifa, ili hatimaye, wananchi waweze kujenga na kuimarisha utamaduni wa amani. Umefika wakati wa kuvumiliana na kujenga mazingira yatakayoweza kuufanya mchakato mzima wa uchaguzi kuwa huru na wa haki, kwa kujenga na kuimarisha amani na utulivu. Vurugu na vitisho ni sumu kali dhidi ya demokrasia na utawala wa sheria.








All the contents on this site are copyrighted ©.