Maaskofu Kenya wanawatakia Wakenya wote: Umoja, Amani na Uhuru wa kweli!
Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, anaendelea kuwahimiza
wananchi wa Kenya na Vyama vya Kisiasa kwa ujumla kuhakikisha kwamba, vinatoa nafasi
kwa Mahakama kuu kuweza kutekeleza wajibu wake barabara baada ya mmoja wa wagombea
uchaguzi mkuu uliopita nchini humo kukata rufaa kupinga matokeo ya Urais.
Kardinali
Njue amemwomba pia Rais kukubaliana na masharti yaliyotolewa na Mahakama kuu ya Kenya,
kama sehemu ya utekelezaji wa utawala wa sheria. Ni wajibu kwa vyama vya kisiasa wakati
huu tete nchini Kenya, kujizuia kufanya maandamano yanayoweza kuleta vurugu na uvunjifu
wa amani nchini Kenya. Hii inatokana na ukweli kwamba, wananchi wa Kenya wamechoshwa
na vurugu na kinzani za kijamii, na wala si busara tena kuwashirikisha katika masuala
ambayo wanapenda kuyapatia mgongo na kuanza ukurasa mpya wa maisha na maendeleo yao.
Shirika
la Habari za Kanisa kutoka Afrika, CISA linasema kwamba, Maaskofu Katoliki Kenya wanawapongeza
wananchi wa Kenya kwa kujitokeza kwa wingi kutekeleza haki yao msingi kama raia kwa
kupiga kura kwa amani na utulivu, huku wakivumiliana kutokana na tofauti zao za kisiasa,
dalili za ukomavu wa kidemokrasia. Maaskofu pia wanawapongeza Wakenya kwa kuonesha
uvumilivu na busara wakati wa kuhesabu kura na hatimaye, matokeo yalipotangazwa, hii
inaonesha kwamba, kwa hakika Wakenya ni wapenda amani.
Maaskofu wanavishukuru
na kuvipongeza vyombo vya ulinzi na usalama, kwa kuonesha umakini katika mchakato
wa uchaguzi mkuu; wanawapongeza wanasiasa walioshiriki katika uchaguzi mkuu na vyama
vya kisiasa kwa ujumla wao. Wanawapongeza wale ambao tayari wamekubali kushinda na
kushindwa katika uchaguzi uliopita na kwamba, vyombo vya upashanaji habari vimetekeleza
wajibu wao barabara.
Askofu mkuu Zacchaeus Okoth wa Jimbo kuu la Kisumu, Kenya
anasema, Maaskofu walikuwa na wasi wasi wa ujumbe na matamshi yalionesha chuki na
uhasama wa kikabila yaliyokuwa yamezagaa kwenye mitandao yao ya kijamii. Inasikitika
kuona kwamba, bado kuna chembe chembe za chuki za kikabila. Anawataka kuongozwa na
dhamiri nyofu, daima wakitafuta na kudumisha tunu msingi zinazopewa kipaumbele na
Nchi ya Kenya katika ujumla wake.
Maaskofu wanaendelea kukazia umuhimu wa
kudumisha misingi ya haki, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa, wakati huu wanaposubiri
uamuzi wa Mahakama kuu. Wakati huu wa Juma kuu na hatimaye, Kipindi cha Pasaka, iwe
ni fursa ya kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa; upendo pamoja na
uchaji wa Mungu. Maaskofu wanatakia wakenya umoja, amani na uhuru wa kweli mioyoni
mwao!