Mashirika ya kilimo na chakula ya Umoja wa Mataifa kuendeleza ushirikiano na Tanzania
Waziri mkuu Mizengo Pinda wa Tanzania, amekutana na wakuu wa taasisi za kimataifa
za WFP, IFAD na FAO na kufanya nao mazungumzo kuhusu namna ya kuendeleza kilimo nchini
Tanzania.
Waziri Mkuu amekutana na viongozi hao Machi 21, 2013 alipowatembelea
kwenye ofisi zao jijini Roma, Italia kila mmoja kwa nyakati tofauti.
Mkurugenzi
Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mtaifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), Bi. Ertharin
Cousin, alimweleza Waziri Mkuu kwamba shirika lake litaendelea kutumia bandari ya
Dar es Salaam kusafirishia vyakula kwenda nchi zenye uhitaji wa chakula ikiwa ni utekelezaji
wa mpango wa ununuzi wa bidhaa kwa maendeleo (Purchase for Progress Programme).
“Tumekubaliana
na wadau tunaoshirikiana nao, tuendelee kutumia bandari ya Dar es Salaam kupeleka
mizigo Sudan ya Kusini na Uganda kwa sababu ya amani iliyopo nchini Tanzania. Kwa
hiyo muamini kwamba sisi ni wadau wenu wa karibu na wa kuaminika,” alisema Bi. Cousin.
Akitoa
mfano, Bi. Cousin alisema: “Kuna wakati kulikuwa na njaa kubwa kule Somalia na Zambia
wakawa na hifadhi kubwa ya mahindi, lakini tulishindwa kusafirisha mahindi kutoka
huko na kuyapeleka yanakohitajika kwa sababu ya hali mbaya ya usalama kwenye ukanda
wa magharibi,” alisema.
Akizungumzia kuhusu ukuaji wa miji na kasi ya watu
kuhamia mijini, Bi. Cousin alionya kwamba kuna haja ya kuwianisha uendelezaji wa miundombinu
kwenye maeneo ya mijini na yale ya vijijini ili kuepuka tatizo la msongamano mkubwa
wa watu mijini linalozikabili nchi nyingi zinazoendelea.
Alisema shirika lake
limefanya utafiti nchini India na kubaini kuwa kadri kiwango cha ukuaji wa miji kinavyoendelea
ndivyo kasi ya wakazi kuongezeka inavyozidi. “Tumeziainisha nchi za Kenya, Tanzania
na Ethiopia na kuziweka kwenye mpango maalum ili zijipime jinsi zitakavyokuwa katika
miaka 20 ijayo ili zisije kuwa na hali kama ya India hivi sasa,” aliongeza.
Naye,
Rais wa Shirika la Kimataifa Kuendeleza Kilimo na Chakula (IFAD), Dk. Kanayo Nwanze
alimweleza Waziri Mkuu kwamba shirika lake limeandaa mpando wa miaka mitatu ambao
utazihusisha nchi 30 ikiwemo Tanzania ambazo zitafanyiwa impact evaluation kulingana
na misaada ambayo zimekuwa zikipatiwa na shirika hilo.
“Tunataka tuangalie
hali halisi kule Vijijini, Je, maisha ya wananchi yamebadilika kulingana na misaada
ambayo tumekuwa tukiitoa? Je, wakulima wameongeza uzalishaji? Je wakulima wameunganishwa
na masoko? Je, taasisi za kifedha zinawajali wakulima wadogo?” alifafanua Rais huyo
wa IFAD.
Alisema hivi sasa wameanza kukusanya takwimu za awali (baseline data)
katika nchi husika kabla ya kuanza kufanya tathmini itakayoanza mwaka huu hadi mwaka
2016.
Mapema, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na
Kilimo (FAO), Bw. Jose Graziano da Silva alimweleza Waziri Mkuu kwamba shirika lake
limetiliana saini makubaliano na benki ya Rabo (Rabobank) ili iweze kuwasaidia wakulima
waliojiunga kwenye vyama vya ushirika.
“RaboBank imekubali kufanya kazi hiyo
na imeichagua Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zitakazokuwa waanzilishi wa mpango huo
(pilot project)… watawasiliana nanyi muda si mrefu kuhusiana na suala hili,” alisema.
Aliomba
wakati mpango huo utakapoanza, wakulima wa Tanzania wawe tayari kushiriki kwenye mpango
huo.
Waziri Mkuu Pinda kwa upande wake, katika nyakati tofauti aliwaarifu wakuu
wa taasisi hizo za kimataifa juu ya hali ya uchumi wa Tanzania, Mpango wa Kuendeleza
Sekta ya Kilimo (ASDP), Ukanda wa Kilimo wa Nyanda za Juu Kusini (SAGCOT) na mchakato
wa kuandaa Katiba mpya.
Alisema ili kuendeleza kilimo, ipo haja ya kushirikiana
na wadau kutoka sekta binafsi kama njia ya kuleta maendeleo ya haraka nchini Tanzania.
Bado tunayo changamoto ya kukabiliana na umaskini, lakini tunaamini kuwa kilimo ndiyo
jawabu la tatizo hili,” alisema.
Waziri Mkuu alikwenda Roma, Italia kumwakilisha
Rais Jakaya Kikwete kwenye ibada maalum ya kumsimika Papa Francis iliyofanyika Jumanne,
Machi 19, 2013 kwenye Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, kisha
akaamua kukutana na viongozi wa taasisi hizo.
Hii ni taarifa iliyotolewa na
Ofisi ya Waziri mkuu kwa vyombo vya habari.