2013-03-21 13:19:23

Alhamisi kuu, Papa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Gereza la watoto wadogo!


Baba Mtakatifu Francisko, katika maadhimisho ya Alhamisi kuu hapo tarehe 28 Machi 2013, Mama Kanisa anapofanya kumbu kumbu ya siku ile iliyotangulia kuteswa kwake Kristo, alipoweka Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, Daraja Takatifu la Upadre, Sakramenti zinazofumbatwa katika huduma kwa Mungu na jirani; jioni saa 11:30 saa za Ulaya, ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Gereza la Watoto hapa mjini Roma.

Itakumbukwa kwamba, Ibada ya Misa Takatifu Alhamisi kuu jioni, inakazia kwa namna ya pekee huduma ya upendo, inayojionesha kwa Kristo kwa kuwaosha wanafunzi wake miguu, changamoto ya kuendeleza huduma hii, kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Baba Mtakatifu Francisko katika utumishi wake kama Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires, alizoea kuadhimisha Ibada ya Alhamisi kuu, Hospitalini au Gerezani, kama kielelezo cha huduma ya upendo wa Kristo kwa wale wanaojisikia kuwa wanyonge mbele ya macho ya walimwengu.

Baba Mtakatifu Francisko anapenda pia hata katika dhamana yake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, kuendeleza utume huu miongoni mwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Ibada za Juma kuu hapa mjini Vatican zitaendelea kadiri ya utaratibu kutoka kwa Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa.

Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Benedikto XVI alitembelea Gereza la Watoto Wadogo, "Casal del Marmo" tarehe 18 Machi 2007 na kuadhimisha Ibada ya Misa takatifu katika Kikanisa cha Baba Mwenyehuruma kilichoko kwenye taasisi hiyo.







All the contents on this site are copyrighted ©.