2013-03-19 10:04:17

Papa Francisko aanza utume wake rasmi kama Khalifa wa Mtakatifu Petro na Askofu wa Roma


Baba Mtakatifu Francisko ameanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, wakati huu Kanisa linapoadhimisha Siku kuu ya Mtakatifu Yosefu, Baba mlishi wa Yesu na mchumba safi wa Bikira Maria. Kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, Baba Mtakatifu Francisko anakuwa pia ni Askofu wa Jimbo la Roma, Kanisa ambalo ni kielelezo cha upendo na mshikamano na Makanisa mengine yaliyoenea sehemu mbali mbali za dunia.

Ibada ya kuanza kwa utume wa Khalifa wa Mtakatifu Francisko imesheheni utajiri mkuu wa mafumbo ya imani.

Ibada ya Fumbo la Ekaristi Takatifu imeadhimishwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mahali ambapo kadiri ya Mapokeo, Mtakatifu Petro aliyamimina maisha yake kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.

Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro na viunga vya mji wa Vatican, vimesheheni watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, waliofika mjini Vatican kushuhudia tukio hili la kihistoria. Takwimu zinazonesha kwamba, zaidi ya viongozi wakuu wa nchi 132 wamehudhuria. Kuna wawakilishi wa dini na madhehebu mbali mbali waliofika pia kuonesha moyo wa upendo na mshikamano katika kumhudia mwanadamu katika hija ya maisha yake ya kiroho hapa duniani.

Baba Mtakatifu Francisko ameanza tukio hili kwa kuzunguka na kuwasalimia waamini, mahujaji na watalii waliofika kumshuhudia akianza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro na Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Roma. Baadaye, Baba Mtakatifu alirudi kwenye Sakristia ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, kujiandaa kwa ajili ya maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu. Alipokuwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, alishuka kwenye gari lake na kuenda kumsalimia mgonjwa aliyekuwa amebebwa na ndugu zake, waliokuwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu pamoja na wahusika na wawakilishi walishuka kwenye Kaburi la Mtakatifu Petro, chini ya Altare kuu ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, akapata muda wa kusali na kutafakari kidogo, wakati huo, tarumbeta zilikuwa zinapigwa kuonesha kwamba, Khalifa wa Mtakatifu Petro ameanza hija ya utume wake rasmi. Baba Mtakatifu amevikwa Palio takatifu, Pete ya Ukulu wa Mtakatifu Petro ambayo si ya dhahabu na Injili ambayo ilikuwa imewekwa kwenye Kaburi la Mtakatifu Petro, usiku uliokuwa umetangulia.

Baadaye, Baba Mtakatifu pamoja na Makardinali na Maaskofu wakuu kutoka Makanisa ya Mashariki walipanda kuelekea kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, wakati wote huo, Waamini walikuwa wanaimba wimbo wa kumsifu Kristo Mfalme, wakitumia baadhi ya maneno yalitolewa kwenye Mtagsuo Mkuu wa Pili wa Vatican. Litania ya Watakatifu iliimbwa.

Baba Mtakatifu ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu alisaidiwa na wakuu wawili wa Mashirika ya Kitawa: Mheshimiwa Padre Josè Rodriguez Carballo, Mkuu wa Shirika la Wafranciskani pamoja na Padre Adolfo Nicolas Pachon, Mkuu wa Shirika la Wayesuit. Kabla ya Ibada ya Misa Takatifu, Baba Mtakatifu alivishwa Palio takatifu na Kardinali, shemasi Tauran, baadaye alivishwa Pete ya Mvuvi na Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali. Baadhi ya Makardinali waliwawakilisha Makardinali wenzao kuonesha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro.







All the contents on this site are copyrighted ©.