Serikali ya Tanzania yaombwa kukomesha vurugu za kidini na madhulumu kwa viongozi
wa kidini
Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro amemwelezea Rais Jakaya Mrisho Kikwete
kama kiongozi anayelijali Kanisa Katoliki Tanzania na mwenye nia njema. Aidha, Kanisa
hilo limesema kuwa Rais Kikwete amethibitisha katika muda wake wote wa uongozi wa
Taifa la Tanzania kuwa ni kiongozi ambaye anawajali wanyonge na maskini.
Sifa
hizo za kulijali Kanisa Katoliki na kuwa na nia nzuri na Kanisa hilo zilitolewa usiku
wa Alhamisi, Machi 14, 2013 na Askofu Telesphor Mkude wakati wa hafla ya kuchangia
ujenzi wa Parokia mpya ya Kigurunyembe iliyofanyika kwenye Bwalo la Jeshi la Wananchi
wa Tanzania la Magadu Officer’s Mess, nje kidogo ya mji wa Morogoro.
Akitoa
neno la shukrani wakati akimkaribisha Rais Kikwete kwenye hafla hiyo na baada ya kukamilika
kwa shughuli ya uchangiaji, Askofu Mkude alimwambia Rais Kikwete “Wewe Mheshimiwa
Rais ni kiongozi ambaye unalijali Kanisa Katoliki. Una nia nzuri na Kanisa. Kigurunyembe
ni sehemu ndogo sana ya nchi ya Tanzania ambayo wewe unaiongoza. Hata hivyo, umekuwa
tayari kuacha yote yaliyo makubwa na kukubali kujishusha na kuja kuzungumza na hili
kundi dogo la Kigurunyembe.”
Aliongeza Baba Askofu Mkude: “Kwa hili unatufundisha
kwa vitendo maana ya kujali wanyonye na maskini. Baba Mheshimiwa umetujali sana. Mungu
akubariki sana.” Alisisitiza Askofu Mkude: “Mwisho mgeni rasmi nirudie kwa kukushukuru
na kusema kuwa yote haya yasingeliwezekana kama usingeliwepo wewe mwenye binafsi kwenye
shughuli hii. Tunakushukuru kwa kutujali, kututhamini na kutupenda sisi kama raia
wa nchi yako na ukaona ni bora ufike mwenyewe.”
Uchangiaji huo wa ujenzi wa
parokia mpya ya Kigurunyembe ulilenga kukusanya kiasi cha Sh. Milioni 200 lakini wachangiaji
waliishia wakichangia kiasi cha Sh. Milioni 255 zikiwamo fedha taslim Sh. Milioni
73.
Katika neno lake, Askofu Mkude pia aliwashangaa watu ambao wamekuwa wanachoma
makanisa nchini kwa visingizio vya dini akisema kuwa taasisi na majengo yanajengwa
kwa thamani kubwa na kama kweli Watanzania wanapenda maendeleo ni lazima waache kuchoma
majengo yanayojengwa kwa thamani kubwa.
“Mtapata wapi maendeleo kwa kuchoma
taasisi na majumba ambayo tayari tumeyajenga tena kwa gharama kubwa sana?” aliuliza
Askofu Mkude na kumtaka Rais Kikwete kuchukua hatua za kukomesha fujo na vurumai za
kidini nchini pamoja na kuuawa kwa viongozi wa dini.
“Haya siyo mazoea yetu
kama ulivyosema wewe Mheshimiwa Rais katika hotuba yako ya mwezi Januari mwaka huu.
Huu siyo utamaduni wetu. Ni lazima tukubali kurudi kuishi katika haki, katika amani
na katika heri. Tunakuomba utusaidie makanisa yetu yasichomwe moto. Utusaidie viongozi
wetu wasiuawe Mheshimiwa Rais.”