2013-03-16 09:10:31

Papa Francis ni Baba wa Maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii


Kardinali Oscar Rodriguez Maradiaga, Rais wa Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis anampongeza Baba Mtakatifu Francis kwa kuchaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, kwa waamini wapatao Billioni 1.2, walioenea sehemu mbali mbali duniani, baada ya siku mbili za kikao cha Conclave kilichokuwa kinafanyika kwenye Kikanisa cha Sistina, mjini Vatican.

Caritas Internationalis inaungana na Watu wa Familia ya Mungu kusali kwa ajili ya kumwombea Baba Mtakatifu Francis, ina Sali pia kwa ajili ya ulimwengu mzima, ili kujenga na kuimaarisha mshikamano wa kidugu miongoni mwa Jumuiya ya Kimataifa.

Caritas inasema kwamba, Papa Francis ni Myesuit wa kwanza kabisa kuwahi kuchaguliwa kuwa Papa tangu Shirika hili lilipoanzishwa na Mtakatifu Inyasi wa Loyola. Ni Kiongozi wa kwanza kabisa katika historia ya Kanisa kuchaguliwa kutoka miongoni mwa waamini wa Amerika ya Kusini. Ni kiongozi ambaye amejipambanua kwa kuchangia huduma kwa maskini na wote wanaosukimizwa pembezoni mwa Jamii. Ameonesha upendo wa pekee kwa wagonjwa na waathirika wa Ukimwi, kiasi cha kuwaosha miguu kwa upendo wa kibaba.

Kardinali Oscar Maradiaga anasema, si bure kujitwalia jina la Mtakatifu Francis, kwani Francis wa Assisi alijimbanua kwa mshikamano wake makini na thabiti kwa maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii, kiasi hata cha kuacha utajiri na fahari ya nyumbani kwake, ili kushiriki katika ujenzi wa Kanisa la Kristo, kwa njia ya huduma makini na ya kina kwa maskini wa nyakati zake.

Caritas inaona kwamba, hapa kwa hakika “upele umepata mkunaji”. Papa Francis anatarajiwa kuwa mdau mkuu katika kutafuta, kutetea na kudumisha haki jamii, kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Ni changamoto ya kuendelea kudumisha haki, amani, umoja na udugu, kama alivyosema Papa Francis alipoonekana hadharani kwa mara ya kwanza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro na Baba wa Mataifa. Itakumbukwa kwamba, Caritas ni mdau mkubwa wa huduma ya upendo inayotolewa na Mama Kanisa sehemu mbali mbali za dunia, bila ubaguzi, kwani wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.








All the contents on this site are copyrighted ©.