2013-03-16 16:47:10

Dira: Usiwasahau Maskini, dumisha amani na utunzaji bora wa mazingira!


Baba Mtakatifu Francis, Jumamosi, tarehe 16 Machi 2013 amewashukuru na kuwapongeza wanahabari kutoka sehemu mbali mbali za dunia ambao wamekuwa wakifuatilia matukio muhimu ya Kanisa tangu pale Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alipoamua kwa utashi na uhuru kamili kung'atuka kutoka madarakani. Amepongeza kazi kubwa inayofanywa na vyombo vya mawasiliano ya Jamii katika ulimwengu wa utandawazi.

Baba Mtakatifu Francis anawapongeza wanahabari waliofanya kazi zao usiku na mchana kuwahabarisha watu kile kilichokuwa kinatendeka mjini Vatican, kwenye Kaburi la Mtakatifu Petro. Wamepata nafasi ya kuweza kusimulia kuhusu Vatican, Kanisa, Ibada na Mapokeo yake, Imani; Dhamana na Utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hili ni tukio la imani linalopaswa kutazamwa katika mwono wa imani, ili kuweza kutoa taarifa kamili kwa hadhira inayokusudiwa. Ni tukio kwa ajili ya watu wa Mungu wanaofanya hija ya kumwendea Yesu Kristo. Kwa kuwa na ufahamu huu, ndipo mtu anavyoweza kung'amua mantiki ya maisha na utume wa Kanisa.

Baba Mtakatifu Francis anabainisha kwamba, Kristo ndiye mchungaji mkuu wa Kanisa anayeendelea kuwapo katika historia kwa njia ya uhuru wa binadamu. Kati ya watu wengi, kuna mmoja anayechaguliwa kuwa ni Khalifa wa Mtakatifu Petro, lakini ikumbukwe kwamba, mhusika mkuu ni Yesu Kristo ambaye ni rejea ya Kanisa na bila Kristo hakuna Kanisa na wala akina Petro na ndugu zake wasingakuwepo! Kristo yupo na anaendelea kuliongoza Kanisa lake hadi utimilifu wa dahali.

Baba Mtakatifu Francis anasema kwamba, matukio yote yaliyotendeka ndani ya Kanisa kwa siku za hivi karibuni, mhusika mkuu ni Roho Mtakatifu; ndiye aliyemwongoza Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kung'atuka kutoka madarakani, kwa ajili ya mafao, ustawi na maendeleo ya Kanisa. Anamshukuru kwa uwapo wake kwa njia ya Sala na tafakari ya kina, iliyowaongoza Makardinali wakati wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Kanisa lina asili mbili: ile ya Kimungu na kibinadamu; ina karama na mapungufu yake, lakini linatambua dhamana na wajibu wake katika maisha ya mwanadamu, changamoto kwa wanahabari kujitahidi kuwapatia watu mwanga wa matukio haya, daima wakijitahidi kukumbatia ukweli, matashi mema na uzuri unaolifanya Kanisa kuendelea kutangaza ukweli, utashi na uzuri wa binadamu. Kila mtu anaalikwa kutangaza mambo haya msingi na wala si kujitangaza mwenyewe!

Jina Francis ambalo analitumia anasema ni changamoto iliyotolewa kwake na Kardinali Claudio Hummes, baada ya kuona kwamba, amechaguliwa kuliongoza Kanisa kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, akamwambia, usiwasahau maskini. Hapa wazo la Mtaka Francis wa Assisi likamjia kichwani kwake, kwani ni mtu ambaye alipenda kudumisha amani na utunzaji bora wa mazingira. Mtu ambaye ana moyo na mwelekeo wa namna hii kwa hakika lazima ajikite katika maisha ya ufukara.

Anawataka wanahabari kutekeleza majukumu yao kwa amani na utulivu wa ndani; daima wakijitahidi kuifahamu Injili ya Kristo na hali halisi ya maisha na utume wa Kanisa. Baada ya hotuba yake iliyokuwa inashangiliwa mara kwa mara, Baba Mtakatifu Francis aliwaweka wanahabari waliokuwa wamefurika kwenye Ukumbi wa Paulo wa sita, wakiwa na familia, ndugu na jamaa zao, chini ya uongozi na usimamizi wa Bikira Maria.







All the contents on this site are copyrighted ©.