Kipindi cha Kwaresima kiwasaidie waamini kuwajibika katika utunzaji bora wa mazingira
Jumuiya ya Waanglikani Duniani katika Maadhimisho ya Kipindi cha Kwaresima kwa Mwaka
2013 inawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kulinda, kuheshimu na kutunza
mazingira kwa kupunguza hewa ya ukaa wanayozalisha majumbani, viwandani na maeneo
yao ya kazi, kama sehemu ya mchakato wa kuendeleza kazi ya uumbaji. Itakumbukwa kwamba,
Kwaresima ni muda muafaka uliokubalika wa kufanya: toba na wongofu wa ndani; kufunga
na kusali; kusoma na kulitafakari Neno la Mungu pamoja na kutekeleza matendo ya huruma.
Kipindi cha Kwaresima
ni mwaliko wa kuondokana na mambo yote yanayokwenda kinyume na mapenzi na mpango wa
Mungu kwa mwanadamu na viumbe wengine wote, kwani hata wao pia ni sehemu ya kazi ya
Uumbaji. Waamini wa Kanisa Anglikani kwa namna ya pekee kwa Mwaka huu, wanaalikwa
kujikita zaidi katika matendo ya huruma kutokana na sadaka ambayo wataifanya wakati
wa Kipindi chote cha Kwaresima, Siku Arobaini za kutafakari: Mateso, Kifo na Ufufuko
wa Kristo. Ile ni fursa kwa waamini kuangalia mchango wanaoweza kuchangia katika kudhibiti
athari za mabadiliko ya tabianchi.
Siku arobaini zisaidie kuamsha changamoto
na ari ya kulinda na kutunza mazingira, kama sehemu ya mchakato wa kuenzi kazi ya
uumbaji ambayo Mwenyezi Mungu amemdhaminisha mwanadamu, lakini kutokana na ubinafsi
na matumizi mabaya mazingira, dunia inaendelea kushuhudia athari kubwa za mabadiliko
ya tabianchini. Kufunga na kujinyima ni sehemu ya mapokeo ya kipindi cha Kwaresima.
Waamini wajifunze kujenga na kudumisha utamaduni wa kujinyima na kutoa sadaka kwa
maskini na wahitaji zaidi. Kwa mwaka huu, waamini na watu wenye mapenzi mema, wajifunze
kutoa sadaka kwa kupunguza uzalishaji wa hewa ya ukaa; kwa kufanya mabadiliko makubwa
katika mtindo wa maisha, ili kudhibiti athari za mabadiliko ya tabianchi.
Kwaresima
kiwe ni kipindi cha matumizi bora ya rasilimali ambayo waamini wamekabidhiwa na Mwenyezi
Mungu. Mazingira bora ni kati ya zawadi kubwa ambazo mwanadamu amekabidhiwa, lakini
hatima yake iko mashakani. Ikumbukwe kuwa kila mtu anachangamotishwa kujenga utamaduni
wa kutunza mazingira; watu wajifunze kubana matumizi ya maji wanayotumia, kwani maji
ni uhai. Inawezekana kabisa kupunguza matumizi ya umeme na gasi majumbani na ofisini.
Unaweza kupunguza uzalishaji wa hewa ya ukaa kwa kutumia usafiri wa umma badala ya
kuendesha gari binafsi.
Kwaresima kiwe ni kipindi cha kumrudia Mwenyezi Mungu
kwa moyo mkuu. Yale ya kale yaliyoharibu uhusiano mwema na Mwenyezi Mungu, yazikwe
kwenye majivu wanayopakwa waamini Jumatano ya Majivu. Waamini wakimbilie wema na huruma
ya Mungu kwa njia ya kufunga, toba na matendo ya huruma kwani Mungu ni mwingi wa huruma
na mapendo, atawapokea na kuwasamehe dhambi zao. Kila mtu akithubutu, inawezekana
kulinda na kutunza mazingira, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.