2013-03-15 08:56:24

Changamoto kuu: ni kutembea, kujenga na kumuungama Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka!


Baba Mtakatifu Francis, Alhamisi tarehe 15 Machi 2013, Jioni, ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuliombea Kanisa akishirikiana na Makardinali walioshiriki katika uchaguzi wa Papa Mpya kwenye Kikanisa cha Sistina, mjini Vatican. Katika mahubiri yake kwa mara ya kwanza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro amekazia mambo makuu matatu: kutembea, kujenga na kuungama.

Familia ya Mungu inaalikwa kutembea katika mwanga wa Mungu, kwa kutambua kwamba, maisha ya kila mwanadamu ni hija inayomwajibisha kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yake kama alivyofanya kwa Mzee Ibraham, Baba wa Imani na hatimaye, Mwenyezi Mungu akamtekelezea ahadi zake.

Baba Mtakatifu Francis anasema, waamini lazima wajitambue kwamba wao ni mawe hai na hivyo wanachangamotishwa kulijenga na kuliimarisha Kanisa, wakiwa wameungana na Roho Mtakatifu. Ni mwaliko wa kulijenga Kanisa ambalo ni mchumba amini wa Kristo, juu ya Jiwe kuu la pembeni ambalo ni Kristo mwenyewe.

Familia ya Mungu katika hija ya maisha yake hapa duniani inaalikwa kufanya hija pamoja na Kristo ili kumshuhudia Kristo kwa njia ya sala na matendo thabiti, vinginevyo waamini wanaweza kujikuta wakimtumikia shetani na hatimaye kumezwa na malimwengu.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francis anawaalika waamini kutembea, kujenga, kuimarisha na kushuhudia; dhamana ambayo si rahisi kuitekeleza kutokana na ukweli kwamba, kuna wakati ambapo waamini wanaweza kukumbana na vikwazo pamoja na vizingiti vinavyoweza kuwafanya kushindwa kusonga mbele zaidi. Waamini wajitahidi kuungana na Mtakatifu Petro ambaye alimuungama Yesu kuwa ni Mwana wa Mungu aliye hai, ingawa mwanzoni alitishika kwa uwepo wa Msalaba!

Baba Mtakatifu Francis anasema kwamba, Waamini hawawezi kufanya hija na kupania kulijenga Kanisa bila ya kuukumbatia Msalaba, kwani mwelekeo huu ni kinyume kabisa cha ufuasi wa Kristo, haijalishi wewe una nafasi gani katika Kanisa. Hija ya mfuasi wa Kristo inaambatana na Msalaba. Papa anawaalika Makardinali baada kusali na kutafakari wakati wote walipokuwa kwenye uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, sasa wanapaswa kuwa na ujasiri wa kutembelea mbele ya Kristo kifua mbele huku wakiwa wameukumbatia Msalaba.

Hii ni changamoto ya kulijenga Kanisa juu ya Damu Azizi ya Yesu iliyomwagika pale juu Msalabani; kuungama ukuu wa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka, kwa njia hii Kanisa litazidi kusonga mbele. Baba Mtakatifu Francis amewatakia Makardinali wote nguvu ya Roho Mtakatifu kwa maombezi ya Bikira Maria, ili kwa pamoja waweze kutembea, kujenga na kumshuhudia Yesu Kristo Mteswa!

Katika sala za Waamini, Kanisa limesali kwa ajili ya kumwombea Khalifa wa Mtakatifu Petro Mpya pamoja na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, ili aendelee kulihudumia Kanisa katika maisha ya sala na tafakari. Wamewaombea viongozi wa kimataifa kutumia vyema madaraka yao kwa ajili ya mafao ya wengi na wala si kwa ajili kujitafuta wenyewe au kwa ajili ya mafao yao binafsi. Kanisa limewaombea pia wale wote wanaoteseka sehemu mbali mbali za dunia, ili waweze kufarijiwa na hatimaye, kupewa taji la utukufu.

Mara baada ya Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, Papa Francis alikwenda kutembelea makazi yake mapya ambayo kwa sasa yanaendelea kufanyiwa ukarabati mdogo.







All the contents on this site are copyrighted ©.