2013-03-13 08:25:29

Wasindikizeni Makardinali kwa njia ya sala ili Kanisa liweze kupata Nahodha Mpya atakayeliongoza Kanisa!


Askofu Richard Smith, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Canada anawaalika waamini nchini humo kuungana na waamini wengine duniani kwa ajili ya kusali ili kuombea mafanikio katika mchakato wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro; ili Kanisa liweze kumpata kiongozi atakeyafaa kuendeleza Jahazi la Mtakatifu Petro, baada ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kuamua kwa utashi na uhuru kamili kung'atuka kutoka madarakani.

Askofu Smith anawaambia waamini nchini Canada kwamba, katika kipindi hiki cha uchaguzi wa Papa Mpya, watasikia mengi, lakini jambo la msingi kwa wao ni kulichukulia tukio hili kwa jicho la imani, kwa kusali na kutafakari dhamana ya Khalifa wa Mtakatifu Petro katika maisha na utume wa Kanisa.

Ni wajibu wao kuwaombea Makardinali ili waweze kuwa na ujasiri wa kumchagua yule ambaye atakabidhiwa funguo za ukulu wa Mtakatifu Petro; kwa kutambua kwamba, Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kielelezo cha umoja na mshikamano wa Kanisa. Ni kiongozi ambaye atakuwa na dhamana ya kuwafundisha: Imani, Maadili na Sala.

Kardinali atakayedhaminishwa dhamana ya kuwa ni Khalifa wa Mtakatifu Petro wa 265, atapaswa kuwa ni kielelezo cha ushuhuda makini wa imani na changamoto ya kutubu na kuongoka. Matukio yote haya yanayoendelea ndani ya Kanisa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, yawaimarishe waamini katika: Sala, Tafakari na Matendo ya huruma; wajitahidi kushikamana zaidi katika kipindi hiki cha neema.







All the contents on this site are copyrighted ©.