2013-03-13 07:47:04

Macho ya waamini yameelekezwa kwenye Kikanisa cha Sistina


Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumanne tarehe 12 Machi 2013 ulifurika umati wa waamini, mahujaji na watalii kushuhudia Makardinali wakila kiapo na hatimaye kuanza mkutano wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Licha ya hali mbaya ya hewa, lakini waamini wakiwa na miamvuli yao, waliendelea kusubiri kwa hamu kufahamu walau matokeo ya kwanza ya uchaguzi wa Papa Mpya.

Ilikuwa ni saa 1: 41 Usiku, kwa saa za Ulaya, sauti kubwa ilipotanda Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kwa kuona moshi mweusi, dalili kwamba, bado Makardinali walikuwa hawajafulu kumchagua Papa Mpya.

Makardinali 115 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura, Jumatano wameendelea na ratiba yao kama kawaida kwa kupiga kura mara nne, yaani kura mbili asubuhi na kura nyingine mbili nyakati za jioni. Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya mawasiliano yamewawezesha mamillioni ya waamini na watu wenye mapenzi mema kufuatilia mchakato wa uchaguzi wa Baba Mtakatifu moja kwa moja kutoka katika Kikanisa cha Sistina, tangu pale Makardinali walipoanza maandamano kutoka kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Paulo, walipoingia kwenye Kikanisa cha Sistina, wakaanza kula kiapo hadi pale Monsinyo Guido Marini alipofunga lango la Kikanisa cha Sistina, ili kutoa nafasi kwa Makardinali kuanza rasmi mchakato wa kupiga kura.

Kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, kuliwekwa Televisheni kubwa nne, zilizowawezesha waamini kufuatilia hatua kwa hatua mchakato mzima wa Conclave, hadi pale moshi mweusi ulipotoka. Ilikuwa ni nafasi kwa waamini pia kuwatambua Makardinali kwa sura kwani wengi wao wamesikika kwa majina, lakini ni wachache waliokuwa wanafahamika zaidi. Katika matukio kama haya havikosekani vituko! Lakini, macho na imani ya watu wengi ni kufahamu nani kati ya Makardinali amechaguliwa kuliongoza Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.