2013-03-12 08:26:52

Macho ya waamini na watu wenye mapenzi mema yanaelekezwa kwa sasa mjini Vatican


Katika mchakato wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, hadi sasa kuna jumla ya Makardinali 152 kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Katika kipindi hiki cha Conclave Makardinali watakaomsaidia Camerlengo ni: Kardinali Antonios Naguib, kutoka katika kundi la Makardinali Maaskofu, Kardinali Marc Ouellet kutoka kundi la Mapadre na Kardinali Francesco Monterisi kutoka katika kundi la Mashemasi.

Padre Federico Lombardi anasema mkutano wa mwisho kabla ya Makardinali kuingia kwenye mchakato wa kumchagua Papa Mpya umezungumzia umuhimu wa ukweli na uwazi katika masuala ya fedha na kwa namna ya pekee, Benki ya Vatican.

Hii ni mada iliyopembuliwa na Kardinali Tarcisio Bertone, ambaye kwa wadhifa wake ni Rais wa Dekania ya Makardinali wanao ratibu shughuli za taasisi hii. Kwa sasa kuna mpango wa kimataifa unaoratibu shughuli za Benki ya Vatican, ili kukazia ukweli na uwazi katika masuala ya fedha.

Makardinali wameendelea pia kupembua wasifu wa Papa Mpya na Matarajio ya Kanisa baada ya uchaguzi huu ambao unafuatiliwa na waamini wengi kwa njia ya sala, lakini pia kwa njia ya vyombo vya upashanaji habari. Makardinali wakishamaliza dhamana ya kupiga kura na hatimaye kumchagua Khalifa Mpya wa Mtakatifu Petro, moshi mweupe utatoka kwenye Kikanisa cha Sistina na hapo kengele za Kanisa kuu la Mtakatifu Petro zitapigwa kuwaalika waamini kuja kusikiliza na kumwona Papa Mpya. Tangu kengele zitakapopigwa hadi Papa Mpya kuonekana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, ni walau muda wa saa moja.

Itakumbukwa kwamba, kuna jumla ya Makardinali 115 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura wakati wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Bado waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee, kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea ufanisi katika uchaguzi wa Papa Mpya unaoanza rasmi tarehe 12 Machi 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.