Hatua za mwisho mwisho kabla ya Papa Mpya kutokeza hadharani!
Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, uchaguzi wa Khalifa
wa Mtakatifu Petro unakamilika kwa Kardinali kupata theluji mbili ya kura zote halali
zilizopigwa. Baada ya hapo, Dekano wa Makardinali ambaye wakati wa uchaguzi ni kardinali
Giovanni Battista Re, atamuuliza Kardinali aliyechaguliwa kama anakubali kisheria
kwamba, amechaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Baada
ya hapo, ataulizwa jina ambalo atalitumia katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu
Petro. Wakati wote huu, Mshehereheshaji mkuu wa Papa ndiye atakayekuwa anachukua rasmi
taarifa zinazotolewa na Papa Mteule akisaidiwa na Washereheshaji wengine wawili wanaokuwepo
mahali hapo kama Mashahidi. Sehemu hii ya mchakato ikikamilika, hapo karatasi zilizotumika
kwa ajili ya kupigia kura zinachomwa na hapo moshi mweupe unatoka kuashiria kwamba
Kanisa limempata Papa Mpya.
Papa Mpya ataelekea kwenye "Chumba cha machozi"
neno ambalo pengine linaonesha ile hali ya ndani anayokuwa nayo Kardinali baada ya
kuambiwa kwamba, amechaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu
Petro. Anaporudi kwenye Kikanisa cha Sistina, Injili inayozungumzia Ukulu wa Mtakatifu
Petro inasomwa, Makardinali wanasali kwa kitambo kidogo na hapo Makardinali moja baada
ya mwingine wanaanza kwenda kula kiapo cha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro, wakati
wote huu, Makardinali na Papa wanaendelea kumshukuru Mungu kwa kuimba utenzi wa shukrani,
Te Deum.
Padre Lombardi anasema, Papa Mpya kabla ya kwenda kwenye Uwanja wa
Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kutoa baraka zake kwa mji wa Roma na Ulimwengu kwa ujumla,
"Urbi et Orbe" atapitia kwanza kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Paulo kusali kwa kitambo
kifupi na baadaye atawasalimia na kuwapatia baraka zake za kitume waamini, mahujaji
na wote watakaokuwa wamekusanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro.
Papa mpya ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kusimikwa kwake, siku yoyote
inayoonekana inafaa zaidi!