Wanawake wanachangamotishwa kuwa waaminifu kwa wenzi wao wa ndoa pamoja na familia
zao!
Mke wa Waziri Mkuu, Mama Tunu Pinda amewataka akinamama wanaojihusisha na shughuli
za ujasiriamali kuwa waaminifu kwa wenza wao na wanafamilia wao ili waweze kupata
ushirikiano kutoka kwao.
Alisema mbali ya majukumu mengi yanayowakabili, akinamama
wanapaswa kuwa karibu na familia zao kwani ndiyo msingi mkuu wa Taifa. “Hatuna budi
kutoa malezi mema kwa wenza wetu na watoto wetu. Tunapofanikiwa katika shughuli zetu,
tusiache kuwa waaminifu kwa wana-familia wetu (akinababa na watoto wetu); tuwaheshimu
na kuwaenzi kwa kuwashirikisha kazi tunazofanya ili tuweze kupata ushirikiano wao
na baraka zao,” alisema.
Mama Pinda ametoa kauli hiyo Jumamosi, Machi 10,
2013 wakati akizungumza na wanawake wajasiriamali walioshiriki Maonyesho Maalum ya
Batik (Batik Gala Night) ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani
kwenye ukumbi wa Hellenic Club, Upanga jijini Dar es Salaam.
Maonyesho hayo
yaliandaliwa na Kamati ya Tamasha la Wanawake Wajasiriamali Tanzania (MOWE) kwa kushirikiana
na Ofisi ya Shirika la Kazi Duniani hapa nchini (ILO) yalikuwa na nia ya kuamsha chachu
ya kuendeleza kazi za akinamama wanaofanya maonyesho kila mwaka yaliyopangwa kufanyika
Oktoba, mwaka huu kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja.
Alisema akinamama wanapaswa
kuungana kwenye vikundi vya ujasiriamali ili waweze kuunganisha ujuzi, stadi walizonazo
na kushirikishana uzoefu. Alisema hawana budi kuhakikisha kuwa bidhaa wanazozalisha
zinakuwa na ubora wa kiwango cha juu ili waweze kukabiliana na ushindani kwenye soko.
“Napenda
kusisitiza, suala la ubora wa bidhaa tunazozizalisha kwa kuzingatia viwango vya Kitaifa
na kimataifa ili bidhaa zetu ziweze kupata uhakika wa soko. Hili litafanikiwa pia
endapo tutazingatia pia ubora wa vifungashio tunavyotumia kwenye bidhaa zetu. Endapo,
tutazingatia viwango, vifungashio na kutumia kiandishi-anuani (barcodes), sioni ni
kwa nini bidhaa zetu zisiende hadi masoko ya mbali huko ughaibuni,” alisema.
Aliwataka
akinamama wajipange vizuri kwa ajili ya Maonyesho makubwa ya kitaifa (MOWE) yatakayofanyika
Oktoba mwaka huu ambayo yatajumuisha washiriki kutoka mikoa yote hapa nchini.
Mapema,
Mkurugenzi wa Shirika la Kazi hapa nchini (ILO Tanzania), Bw. Alexio Musindo, alisema
anawapongeza akinamama wajasiriamali chini ya kamati ya MOWE kwani kupitia mafunzo
yanayodhaminiwa na Ofisi yake, akianamama hao wameweza kujiamini zaidi na kuthubutu
kushiriki maonyesho mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Alisema jamii haina budi
kuwekeza zaidi kwa wasichana kwa kuwapa fursa za kujiendesha kibiashara pamoja na
ujuzi (skills) ili waweze kujiajiri kwani wanakumbana na vikwazo vingi wanapotafuta
ajira ikiwemo, unyanyasaji na unyanyapaa.