2013-03-11 11:53:28

Wanahabari zaidi ya 5,600 wako Mjini Vatican ili kutoa taarifa juu ya mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya!


Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii kwa kushirikiana na Radio Vatican, Kituo cha Televisheni cha Vatican na Idara ya Habari ya Vatican katika ujumla wake, wameanzisha kituo maalum cha huduma za mawasiliano ya Jamii, ili kuwawezesha waandishi wa habari 5,600 kutoka sehemu mbali mbali za dunia kupata habari za uhakika kuhusu mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya unaoendelea hapa mjini Vatican.

Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii linabainisha kwamba, lina uzoefu wa kutosha kufuatia kifo cha Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili sanjari na kutangazwa kwake na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kuwa Mwenyeheri, ni kati ya matukio ambayo yaliwakusanya waandishi wa habari kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wakaridhika na huduma iliyokuwa inatolewa. Kituo hiki cha habari wakati huu wa mchakato wa kumchagua Papa Mpya kimewekwa kwenye Ukumbi wa Paulo wa VI, unaoweza kutoa huduma kwa waandishi wa habari, watangazaji wa Radio na Televisheni pamoja na wapiga picha za kawaida.

Waandishi wa habari waliosajiliwa kwa wakati huu ni kutoka katika nchi 65 wanaowakilisha lugha 24 za kitaifa na kimataifa. Baadhi ya vyombo hivi vya habari vinawasindikiza Makardinali kutoka katika nchi zao, kila chombo kikiwa na lengo lake maalum. Radio Vatican inaendelea kutoa huduma kwa vyombo mbali mbali vya mawasiliano ya Jamii kwa ufanisi mkubwa. Kuna jumla ya vyumba 15 vilivyotengwa maalum kwa ajili ya watangazaji wa radio.

Hadi sasa kuna zaidi ya radio 55 zinazojiunga moja kwa moja na Radio Vatican ili kupata habari za uhakika kutoka hapa mjini Vatican. Vituo vingi vya Radio vinatumia sauti inayotolewa na Radio Vatican pamoja na picha zinazorushwa na Kituo cha Televisheni cha Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.