2013-03-11 08:54:11

Waamini wanasali ili kuombea mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya


Makardinali wanaohudhuria mkutano wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro hapa mjini Vatican, Jumapili iliyopita, tarehe 10 Machi 2013 wameungana na waamini wa Parokia zao za kitume walizokabidhiwa walipokuwa wanasimikwa kuwa Makardinali, kielelezo cha mshikamano na umoja na Askofu wa Jimbo kuu la Roma. Ibada hizi zimehudhuriwa pia na waamini kutoka katika nchi husika.

Lengo ni kuwawezesha Makardinali katika kipindi hiki maalum cha maisha na utume wa Kanisa kutafakari na kusali kwa ajili ya kuombea ufanisi katika uchaguzi wa Papa Mpya ambao unaanza rasmi tarehe 12 Machi 2013. Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar katika adhimisho la Ibada ya Misa Takatifu lililofanyika kwenye Parokia ya Bikira Maria wa Salette alisema kwamba, ustawi na maendeleo ya Kanisa kwa sasa na kwa siku za usoni, umedhaminishwa kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Makardinali kutoka sehemu mbali mbali za dunia wamekusanyika mjini Roma kuanza mchakato wa kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro, utume ambao Mwenyezi Mungu anawakabidhi binadamu, akitumaini kwamba, neema yake itawasaidia kutekeleza wajibu huu msingi, ili Mungu aweze kupata makao miongoni mwa binadamu anayepaswa kuwa kweli ni mdau mkuu katika utekelezaji wa mipango ya Mungu katika kazi ya ukombozi.

Kanisa ambalo ni Fumbo la Mwili wa Kristo, linashirikiana kutekeleza mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu. Khalifa wa Mtakatifu Petro anayo dhamana kubwa ya kuwaongoza Watu wa Mungu kutekeleza wito wao, kwa kutambua nafasi na fursa walizokirimiwa katika kuendeleza historia ya ukombozi wa mwanadamu, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo ambaye kimsingi ni daraja kati ya Mungu na mwanadamu.

Kardinali Peter Erdo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya katika maadhimisho ya Ibada ya Ekaristi Takatifu, Jumapili iliyopita, ameendelea kuwaalika waamini kuisikiliza sauti ya Kristo, mchungaji mkuu, wawe tayari kutubu na kumwongokea Mungu, kama alivyofanya yule Mwana Mpotevu, ili kuonja huruma na upendo wake usiokuwa na kifani. Ni changamoto na mwaliko kwa waamini kuendelea kumshuhudia Kristo kwa maneno na matendo yao adili, ili walimwengu waweze kumwamini Kristo.

Kwa upande wake, Kardinali Angelo Scola wa Jimbo kuu la Milani, amewataka waamini kumwomba Roho Mtakatifu ili aweze kulijalia Kanisa kiongozi makini atakayefuata nyayo za watangulizi wake, yapata miaka 150 iliyopita!.








All the contents on this site are copyrighted ©.