2013-03-11 10:15:59

Uhuru Kenyatta (51) akata mzizi wa fitina nchini Kenya!


Tume huru ya uchaguzi na mipaka imemtangaza Bwana Uhuru Kenyatta (51) kuwa Rais mpya wa Kenya baada ya kushinda uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Kenya hapo tarehe 4 Machi 2013 kwa kumshinda mpinzani wake wa karibu Bwana Raila Odinga. Baada ya kutangaza matokeo ya Urais, Mahakama kuu ina siku 14 za kisheria za kutoa uamuzi juu ya pingamizi lolote dhidi ya matokeo ya urais.

Watu kutoka ndani na nje ya Kenya wanaendelea kuwapongeza wananchi wa Kenya kwa kufanikisha uchaguzi kwa amani na utulivu. Wakati wa Kampeni na hatimaye, uchaguzi wenyewe, viongozi wameonesha ukomavu wa kisiasa kwa kutoa kwanza kabisa kipaumbele kwa mafao ya wengi, ustawi na maendeleo ya wananchi wa Kenya. Huu ni mfano mzuri wa kuigwa na nchi nyingine Barani Afrika.

Mwenyekiti wa Tume huru ya uchaguzi na mipaka anawapongeza wananchi wa Kenya, vyombo vya habari kwa kufanikisha uchaguzi kwa asilimi 86%, hali ambayo imefikiwa kwa mara ya kwanza nchini Kenya.

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya anawashukuru wananchi kwa kumpatia kura ambazo zinamwezesha sasa kuongoza nchi na kutekeleza yale ambayo wameyabainisha katika Ilani ya uchaguzi wa Chama chake. Anaahidi kuwatumikia Wakenya wote katika hali ya usawa sanjari na kuendeleza gurudumu la maendeleo kwa Wakenya wote. Ni matumaini ya Rais Kenyatta kwamba, Jumuiya ya Kimataifa itaheshimu maamuzi ya wananchi wa Kenya waliyoyafanya kwenye uchaguzi mkuu uliopita.

Bwana Raila Odinga anawashukuru wananchi wa Kenya kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mchakato wa uchaguzi mkuu. Anasema ana imani na vyombo vya sheria nchini Kenya, kumbe, atapinga matokeo ya uchaguzi mkuu Mahakamani.

Itakumbukwa kwamba, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya anakabiliwa na mashitaka katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita, ICC, kama ilivyo pia kwa Mgombea mwenza Bwana William Ruto (46). Wanashutumiwa kwa kusababisha machafuko ya kisiasa yaliyopelekea watu kadhaa kupoteza maisha yao mara baada ya matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 kutangazwa.

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alizaliwa kunako tarehe 26 Oktoba 1961. Ni mtoto wa Rais Mzee Jomo Kenyatta na Mama Ngina Kenyatta. Tangu mwaka 2008 alikuwa ni Makamu wa Waziri mkuu wa Kenya. Tangu mwaka 2003 alikuwa ni Mbunge wa Jimbo la Gatundu Kusini. Kunako mwaka 2002 aliteuliwa na Rais Daniel Arap Moi kuwa mgombea Urais kwa tiketi ya KANU, akashindwa katika uchaguzi na Rais Mwai Kibaki. Ni Mwanasiasa Kijana ambaye anashikamana na kijana mwenzake katika kuwaongoza wananchi wa Kenya!







All the contents on this site are copyrighted ©.