2013-03-09 08:05:06

Umaarufu wa Kikanisa cha Sistina wakati wa chaguzi za Mapapa


Kikanisa cha Sistina kimefanyiwa marekebisho ili kuweza kutoa fursa kwa Makardinali kutekeleza wajibu na dhamana nyeti ya kumchagua Baba Mtakatifu Mpya, baada ya Papa Benedikto wa kumi na sita, kwa utashi na uhuru kamili kuamua kung’atuka kutoka madarakani hapo tarehe 28 Februari 2013. RealAudioMP3
Hii itakuwa ni mara ya ishirini na tano kwa uchaguzi wa Papa kufanywa ndani ya Kikanisa cha Sistina chenye utajiri mkubwa wa sanaa. Wakati wote wa mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya, Kikanisa cha Sistina kitakuwa kimefungwa kwa watalii na mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaofika mjini Vatican kushangaa maajabu ya Mungu yaliyotendwa kwa mikono ya wanadamu!
Kunako Mwaka 1996 Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili katika Waraka wake wa Kichungaji kuhusu uchaguzi wa Papa, unaojulikana kama “Universi Dominici Gregis” aliamua kwamba, tangu wakati huo, uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, utakuwa unafayikia ndani ya Kikanisa cha Sistina, ambacho kwa Mwaka 2013 kitatoa nafasi kwa Makardinali 115 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura kushiriki katika uchaguzi wa Papa Mpya.
Itakumbukwa kwamba, Mwaka 1939 Kikao cha Makardinali kilichomchagua Papa Pio wa kumi na mbili, kilianza kutumia kwa mara ya kwanza Jiko ambalo linatumika kwa ajili ya kuchoma kura za Makardinali wakati wa uchaguzi wa Papa Mpya. Hapa ndipo ilipolala siri ya moshi mweupe unaosubiriwa kwa hamu kubwa na waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ambao wanaendelea kufuatilia tukio hili kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya Jamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.