2013-03-09 09:27:32

Makardinali 115 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura kumchagua Papa wa 266 wako tayari mjini Vatican


Mkutano wa nane wa Makardinali uliofanyika Ijumaa tarehe 8 Machi 2013 umewashirikisha Makardinali 153, kati yao Makardinali 115 wana haki ya kupiga na kupigiwa kura. Kardinali Angelo Sodano Dekano wa Makardinali ndiye aliyeongoza mkutano huo, kwa kufafanua baadhi ya vipengele vya Waraka unaohusu uchaguzi wa Papa Mpya, unaowaruhusu kuanza mkutano rasmi baada Makardinali wenye dhamana ya kupiga na kupigiwa kura wanapokuwa wamewasili wote, ikiwa kama hakuna pingamizi au sababu za msingi.

Lakini imefafanuliwa kwamba, zinapopita siku 20 tangu Kiti cha Ukulu wa Mtakatifu Petro kilipoachwa wazi, Makardinali wenye dhamana ya kupiga na kupigiwa kura wanalazimika kuanza mchakato mara moja kadiri ya sheria na kanuni za Kanisa.

Mchakato wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro ni tukio ambalo linafuatiliwa na mamillioni ya watu anasema Padre Federico Lombardi. Makardinali wameanzisha mshikamano wa sala na waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ambao kwa sasa idadi yao ni zaidi ya watu 220, 000, wanaojitoa kwa ajili ya kuwaombea Makardinali katika kipindi hiki wanapojiandaa kwa ajili ya uchaguzi wa Papa Mpya. Kikao cha Conclave kinaanza rasmi Jumanne, tarehe 12 Machi 2013 kwa Ibada ya Misa Takatifu.

Kati ya mambo yanayoendelea kupewa msukumo wa pekee katika mkutano wa Makardinali ni pamoja na majadiliano ya kidini, kiekumene na kitamaduni; maadili, haki na amani katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Wamekazia tasahufi ya huruma na upendo katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kuendelea kuhimiza umoja na mshikamano miongoni mwa Maaskofu wanapotekeleza wajibu na dhamana yao ya kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu.

Makardinali pia wamejadili kuhusu dhamana na mchango wa wanawake katika maisha na utume wa Kanisa. Katika mkutano wa Makardinali, kila Kardinali amepewa nafasi ya kuzungumza mara moja, ili kutoa nafasi kwa Makardinali wengine pia kushirikisha mang'amuzi yao mintarafu utume wa Kanisa la Kiulimwengu.

Padre Lombardi anasema kwamba, Domus Santae Marthae itatumika kama makazi kwa Makardinali wakati wote wa uchaguzi. Mpango na mgawanyo wa vyumba unafanywa na Makardinali wenyewe kwa njia ya bahati nasibu na hakuna Kardinali anayechagua nani aweze kuwa jirani yake au angependelea kuishi katika chumba gani! Papa Mpya atakayechaguliwa kwenye Mkutano wa Makardinali, atalazimika kuishi kwa muda kwenye Hosteli hii, wakati ambapo Jengo la Kitume litakapokuwa limefunguliwa na ukarabati mdogo kufanyika.

Padre Federico Lombardi anabainisha kwamba, licha ya ukweli kuwa Kiti cha Ukulu wa Mtakatifu Petro kiko wazi, lakini Mabaraza ya Kipapa yanaendelea na shughuli zake za kawaida. Kardinali Prospero Grech anatarajiwa kutoa tafakari kwa Makardinali wakati wa mkutano wao.







All the contents on this site are copyrighted ©.