Askofu mkuu Juan Ignacio Arrieta, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la sheria anabainisha
kwamba, wakati ambapo kiti cha Ukulu wa Mtakatifu Petro kinapokuwa wazi, shughuli
msingi za Kanisa zinaendeshwa na Dekania ya Makardinali, lakini kwa maneno machache
ni shughuli zinazoensdeshwa mintarafu sheria na kanuni za Kanisa.
Katika kipindi
hiki, Mabaraza ya Kipapa yanawajibika kutekeleza majukumu yake ya kawaida, kwani kimsingi
anapong’atuka kutoka madarakani kama ilivyokuwa kwa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto
wa kumi na sita, Marais na Wenyeviti wa Mabaraza ya Kipapa nyadhifa zao zinakoma kisheria,
kwani kadiri ya sheria za Kanisa wanakosa rejea na maamuzi ya mwisho yanayopaswa kutolewa
na Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Kwa vile matukio kama haya yanakuja kwa nadra
sana, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican itaendelea kukujuvya taratibu ili uweze
kufahamu walau mambo ya msingi yanayoendelea ndani ya Kanisa kwa wakati huu Makardinali
wanapoendelea na mikutano yao kama sehemu ya mchakato wa kumchagua Papa Mpya wakati
utakapowadia.
Con-clave: neno ambalo litasikika sana wakati huu wa mchakato
wa kumchagua Papa Mpya linatoholewa kutoka katika Lugha ya Kilatini, maana yake, “Kufunga
na ufunguo”. Wakati wa uchaguzi wa Papa Mpya, Makardinali wenye dhamana ya kupiga
na kupigiwa kura hujifungia kwenye Kikanisa cha Sistina kilichoko mjini Vatican.
Hiki
ni kile kipindi kilichokubalika katika kukuza na kuimarisha misingi ya imani, matumaini
na mapendo ya kidugu miongoni mwa Familia ya Mungu; lakini kwa namna ya pekee kwa
Makardinali waliokabidhiwa dhamana ya kushiriki katika mchakato wa kumchagua Khalifa
wa Mtakatifu Petro, kielelezo makini cha imani, matumaini, mapendo, umoja na mshikamano
wa Kanisa.
Uchaguzi wa Papa wakati huu unafanyika katika Kipindi cha Kwaresima
sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili
wa Vatican na Miaka 20 ya Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Haya ni matukio yenye
utajiri mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa. Waamini wanakumbushwa kwamba, hata
kama Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, ameng’atuka kutoka madarakani,
lakini Kristo bado anaendelea kuliongoza Kanisa lake kwa njia ya Roho Mtakatifu na
kamwe haliwezi kuwa ni yatima!
Ni mwaliko kwa waamini kuyaangalia matukio
yote haya kwa jicho la imani na matumaini mintarafu mpango wa Mungu katika maisha
na utume wa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Askofu mkuu
Juan Ignacio Arrieta anasema kwamba, mikutano ya Makardinali iliyoanza tangu Jumatatu
tarehe 4 Machi 2013 inawajumuisha Makardinali wote bila kutofautisha wale wenye haki
ya kupiga na kupigiwa kura. Kimsingi ni mkutano ambao unajadili namna ya kufanya maziko
ya Papa.
Ikumbukwe kwamba, tukio la Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita
kung’atuka kutoka madarakani linafanyika takribani baada ya miaka 600 ya historia
ya Kanisa Katoliki, ndiyo maana watu wengi wamepigwa na bumbuwazi. Kumbe, ni Makardinali
waliokuwa na dhamana ya kusoma Wosia wa Papa aliyefariki dunia na hivyo wanakuwa na
dhamana pia ya kupanga siku ambayo wataanza mchakato rasmi wa uchaguzi wa Papa Mpya.
Hapa neno Conclave, yaani “Con Chiave” kwa lugha ya Kiitalia; Waswahili wakatafsiri
kwa kusema “kufunga na ufunguo” linapata umuhimu wa pekee.
Ni Makardinali peke
yao wanaoruhusiwa kuhudhuria mikutano hii kwani hapa wanalichambua Kanisa “kama karanga”
ili kubainisha hali ya Kanisa, matatizo yaliyopo, fursa na changamoto ambazo wanapaswa
kuzifanyia kazi kwa siku za usoni kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa. Kutokana
na mwelekeo kama huu, hapa Makardinali wanaanza kupata walau “fununu” ya Papa anayetarajiwa
na Mama Kanisa.
Conclave, neno ambalo tutaendelea kulitumia jinsi lilivyo ni
kipindi cha sala. Ndiyo maana Makardinali kila siku jioni wanakutanika kwenye Kanisa
kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ili kusali, kutafakari na kuabudu Ekaristi Takatifu.
Sehemu hii inaongozwa na Sheria za Kanisa kuhusu Liturujia, ili waweze kuongozwa na
Roho Mtakatifu katika uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Lengo ni kuwapatia
Makardinali fursa ya kuweza kusali na kutafakari bila kuwa na haraka, kwani mambo
mazuri hayataki haraka ndivyo wanavyojutuza Waswahili. Ni kipindi ambacho Makardinali
wanajiachilia mikononi mwa Roho Mtakatifu ili aweze kuwaongoza bila kushinikizwa na
watu au sera za makundi ya kijamii.
Papa anayechaguliwa kimsingi ni mtu ambaye
anatarajiwa kuweza kukabiliana na changamoto za Kanisa kwa wakati wake, kama inavyojionesha
pia katika kiapo na kura wanazopiga. Kura zinapigwa mara mbili: ya kwanza inapigwa
asubuhi na kura ya pili inarudiwa jioni, ili kuwapatia Makardinali mwelekeo wa kuamua
ni yupi kati ya wale ambao wamependekezwa anayeweza kwa nguvu ya Roho Mtakatifu kuliongoza
Kanisa.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kunako mwaka 2007 aliamua
kwamba, ili Kardinali aweze kuchaguliwa kuwa Papa lazima apate theluthi tatu ya kura
zote halali na kwamba, Conclave inaweza kufanyika mapema kadiri ya maamuzi ya Makardinali
kwa kusoma alama za nyakati na hivi ndivyo itakavyokuwa.
Sheria na kanuni zinazoongoza
uchaguzi wa Papa Mpya ni nyeti na adhabu yake ni kujitenga na Kanisa mara moja pasipo
na huruma yaani kwa lugha ya sheria za Kanisa hali kama hii inajulikana kama “Latae
Sententiae”. Lengo ni kulinda uhuru wa Makardinali katika mchakato wa kumchagua Khalifa
wa Mtakatifu Petro. Huu ni mwelekeo wa maisha ya kiroho unaooneshwa wakati wa Conclave.
Hapa hakuna ushawishi kutoka nje, kama inavyojionesha kwa sasa, kila upande ukiwapigia
“debe” Makardinali wanaodhani kwamba, wanaweza kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa
wa Mtakatifu Petro.
Ikumbukwe kwamba, kwa Kardinali kuchaguliwa kuliongoza
Kanisa kama Khalifa wa Mtakatifu Petro ni dhamana nyeti inayogusa utume wake. Huu
si “ujiko” au fahari ya mtu. Hivi karibuni kumekuwepo na kampeni kubwa iliyofanywa
na baadhi ya vyombo vya habari kwa kuwachafua watu pamoja na kuwawekea vizingiti kiasi
kwamba, hawataweza kushiriki katika uchaguzi wa Papa Mpya. Hapa waamini wakumbuke
kwamba, huu si uchaguzi wa kisiasa kama wengi walivyozoea.
Kanisa anasema
Askofu mkuu Juan Ignacio Arrieta, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Sheria za Kanisa
kwamba, lina imani na Roho Mtakatifu anatakayewawezesha Makardinali kufanya maamuzi
ya busara pasipokuwa na shinikizo kutoka sehemu yoyote ile!
Na Padre Richard
Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.