2013-03-08 08:33:02

Wanawake simameni kidete: kutetea, kulinda na kueneza Imani kwa Kristo Mfufuka kwa njia ya maisha yenu adili!


Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma, Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, Wanawake Wakatoliki wanayo fursa kubwa ya kuboresha, kuimarisha pamoja na kurithisha imani kwa Kanisa mahalia. RealAudioMP3

Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, wanawake wanakuwa mstari wa mbele: kutetea, kulinda na kuineza imani ya Kristo mfufuka, kama walivyofanya wale wanawake watakatifu wanaosimuliwa kwenye Maandiko Matakatifu.

Ni wanawake waliomsindikiza Yesu katika Njia yake ya Msalaba, wakadiriki kusimama chini ya Msalaba, wakataza mahali alipozikwa, alfajiri na mapema wakaenda kutaka kuutengeneza mwili wake. Ni wanawake hawa watakatifu waliopewa dhamana ya kutangaza ufufuko wa Kristo, pale waliposhuhudia kwa nguvu kwamba, "Kaburi li wazi". Yesu katika maisha na utume wake, aliinua utu na heshima ya wanawake waliokuwa wanadharauliwa katika Jamii kwa wakati ule.

Mfumo dume hata katika Jamii nyingi za Kiafrika bado hautowi nafasi kwa wanawake wengi kushiriki kikamilifu katika maisha ya kijamii hata pengine katika utume wa Kanisa. Kuna haja kwa wanawake kujiamini na kwamba, maadhimisho ya Miaka 40 ya Chama Cha Wanawake Wakatoliki Tanzania, yaliyofanyika hapo mwaka 2012 iwe ni chachu ya kuzaa matunda yanayokubalika, kwa kujikita katika toba na wongofu wa ndani; kwa kutambua na kuthamini ushiriki wao katika kutunza, kutetea na kurithisha imani.

Wanawake hawana budi kuwezeshwa kikamilifu ili waweze kutekeleza utume na dhamana yao kwa Jamii na Kanisa, vinginevyo, Kanisa litaendelea kuchechemea katika kueneza imani, maadili na utu wema, kwani wanawake wanayo nafasi ya pekee kabisa katika utekelezaji wa dhamana hii.

Askofu Michael Msonganzila anabainisha kwamba, kutokana na ukata na hali ngumu ya uchumi, uwepo wa familia tenge na majukumu makubwa wanayowakabili wanawake wengi; vyama vingi vya kisiasa na uelewa tenge wa demokrasia umepelekea wanawake wengi kujikuta wakimezwa na malimwengu. Ikumbukwe kwamba, wakati wa migogoro ya kivita na kijamii, waathirika wakubwa ni wanawake na watoto.

Ni wajibu wa wanawake kusimama kidete kukemea na kulaani vitendo vyote vinavyopelekea kinzani, migogoro na nyanyaso, kwani kila mtu anachangamotishwa kuwa ni mjenzi wa misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli. Ukimwi bado ni janga kubwa kwa Jamii nyingi za Kiafrika na waathirika wakubwa anasema Askofu Msonganzila bado ni wanawake.

Ni changamoto kwa wanawake kusimamia maadili na utu wema, wasikubali kutumbukizwa katika utumwa wa ngono na biashara haramu ya binadamu; mambo ambayo yananyanyasa na kudhalilisha utu na heshima ya wanawake na wasichana.

Wanawake wanapaswa kujifunga kibwebwe kuboresha maisha yao kwa njia halali na wasikubali njia za mkato kwani zinaweza kuwatumbukiza katika madhara makubwa zaidi hata pengine kwa gharama ya maisha na familia zao. Wanawake wapambane kufa na kupona pale inapowezekana ili waweze kujikomboa kiuchumi, kijamii pamoja na kuimarika kiimani. Watambue daima kwamba, hakuna njia ya mkato katika maisha! Kila mtu awajibike kutafuta maisha bora zaidi kwa njia halali!







All the contents on this site are copyrighted ©.