Papa anawashukuru Makardinali kwa upendo, umoja na mshikamano wa kidugu waliomwonesha!
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita ni mtu ambaye anaguswa na matukio
mbali mbali yanayomzunguka na pia ni mtu wa shukrani, hata kwa mambo ya kawaida wanayomtendea
ndugu zake katika Kristo. Ni maneno ya Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican
alipokuwa anaelezea jinsi ambavyo Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita,
alivyopokea ujumbe wa simu ya maandishi kutoka kwa Makardinali kama alama ya shukrani
kwa utume wake kwa Kanisa katika kipindi cha miaka minane, aliyojitoa bila ya kujibakiza
kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Padre Lombardi anasema, ujumbe waliomwandikia
ni mfupi, lakini unaoonesha ule ushuhuda wa upendo na mshikamano wa kidugu pamoja
na uwepo wake endelevu katika maisha na utume wa Kanisa kwa njia ya maisha ya kiroho
yanayofumbatwa katika sala na tafakari ya kina. Idadi kubwa ya Makardinali wenye haki
ya kupiga na kupigiwa kura ni wale walioteuliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi
na sita katika kipindi cha miaka minane ya uongozi wake.
Kwa hakika, anasema
Padre Federico Lombardi, Baba Mtakatifu mstaafu amewashukuru Makardinali kwa kumwonesha
upendo na mshikamano wa kidugu katika kulitumikia Kanisa la Kristo.