2013-03-05 10:54:45

Uchaguzi umekwisha, tulieni kusubiri matokeo!


Askofu mkuu Boniface Lele wa Jimbo kuu la Mombasa hivi karibuni aliwataka waamini na wananchi wa Kenya kwa ujumla kuhakikisha kwamba, wanasimama kidete kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu; kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu.

Wahakikishe kwamba, wanachagua viongozi bora watakaojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wote wa Kenya bila kujikita katika ukabila, udini na umajimbo, kwani haya ni kati ya mambo yanayoweza kukwamisha mchakato wa mageuzi ya kidemokrasia na maendeleo ya wengi. Ni changamoto kwa wananchi wa Kenya kukubali na kuwaheshimu wale watakaoshinda katika uchaguzi mkuu uliofanyika Jumatatu, tarehe 4 Machi 2013 kama kielelezo cha utashi wa wananchi wa Kenya.

Pale ambapo haki haikuzingatiwa, wahusika waitafute haki hii kwa njia za kisheria na wala wasiwatumbukize wananchi katika vurugu na kinzani zisizokuwa na tija wala maendeleo kwa Wakenya. Watu wanasubiri kuona Kenya inayoendelea kusimikwa katika misingi ya amani na umoja wa kitaifa. Mafao ya wananchi wa Kenya hayana budi kupewa kipaumbele cha kwanza, kuliko kitu kingine chochote kile!

Hata katika uchaguzi mkuu wa Mwaka 2013 bado kuna damu ya watu wasiokuwa na hatia imeendelea kumwagika nchini Kenya. Amani na utulivu ni jambo la muhimu sana wakati huu Tume ya Uchaguzi inapoendelea kuhesabu kura kwa njia za kisasa zaidi ili kuongeza kasi ya kuhesabu kura kwa kuzingatia kanuni za ukweli na uwazi, ili kuondoa dhana ya wizi wa kura ambao umekuwa ni wimbo usiokuwa na msikilizaji mara baada ya chaguzi nyingi Barani Afrika.

Taarifa zinabainisha kwamba, wananchi waliojitokeza kupiga kura ni sawa na asilimia 70% ya Wakenya millioni 14.3 waliokuwa wanatarajiwa kupiga kura kwenye uchaguzi mkuu uliomalizika.







All the contents on this site are copyrighted ©.