2013-03-04 07:44:28

Mwenyezi Mungu anatambua mateso na kero za watu wake kiasi cha kuamua kuwa ni mwenza katika hija ya maisha yao!


Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, Jumapili iliyopita, kwenye Parokia ya Bikira Maria wa Salette, iliyoko mjini Roma, ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuombea mchakato wa uchaguzi wa Papa mpya pamoja na kuombea haki, amani na upatanisho Barani Afrika, lakini kwa namna ya pekee, Tanzania ambayo kwa siku za hivi karibuni imekuwa ni uwanja wa dhuluma za kidini.

Kardinali Pengo anasema, ustawi na maendeleo ya Kanisa kwa sasa na kwa siku za usoni, umedhaminishwa kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Makardinali kutoka sehemu mbali mbali za dunia wamekusanyika mjini Roma kuanza mchakato wa kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro, utume ambao Mwenyezi Mungu anawakabidhi binadamu, akitumaini kwamba, neema yake itawasaidia kutekeleza wajibu huu msingi, ili Mungu aweze kupata makao miongoni mwa binadamu anayepaswa kuwa kweli ni mdau mkuu katika utekelezaji wa mipango ya Mungu.

Kanisa ambalo ni Fumbo la Mwili wa Kristo, linashirikiana kutekeleza mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu. Khalifa wa Mtakatifu Petro anayo dhamana kubwa ya kuwaongoza Watu wa Mungu kutekeleza wito wao, kwa kutambua nafasi na fursa walizokirimiwa na Mwenyezi Mungu katika kuendeleza historia ya ukombozi wa mwanadamu, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo ambaye kimsingi ni daraja kati ya Mungu na mwanadamu.

Kardinali Pengo anabainisha kwamba, Maandiko Matakatifu yanamwonesha Mwenyezi Mungu anavyoamua kuchukua nafasi ya mwisho katika maisha ya mwanadamu; kushikamana kwa dhati na maskini, wanyenyekevu wa moyo; wanaodhulumiwa na kunyimwa haki zao msingi; wanaodhalilishwa na utu wao kutwezwa hata kusukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Ni Mungu anayetambua mateso na kero za watu wake, kiasi kwamba, anaamua kuwa ni mwenza katika hija ya maisha yao kwa kuwahakikishia kwamba, kilio cha madhulumu wanayokumbana nayo iko siku kitaweza kusikilizwa; kwani Yeye ni mwenye haki na wakati utakapowadia atayafanya yote mapya.

Kardinali Pengo anasikitika kusema kwamba, katika siku za hivi karibuni, Nchi nyingi za Kiafrika zimekuwa ni uwanja wa madhulumu ya kidini yanayofanywa na baadhi ya waamini wenye misimamo mikali sanjari na matukio ya kigaidi yanayoendelea kupelekea watu wengi wasiokuwa na hatia kupoteza maisha yao. Katika matukio kama haya, Wakristo kwa namna ya pekee, wanaalikwa kuisikiliza ile sauti ya Mungu, ambaye si mwingi wa hasira, bali mpole na mnyenyekevu anayetoa nafasi kwa kila mtu kutubu na kuongoka, ili aweze kuzaa matunda yanayokusudiwa, yaani: haki, amani, upendo na utulivu.

Kanisa kwa kutambua kwamba, linashirikiana na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya mwanadamu, linapenda kuelimisha, kuongoza na kuwasaidia watu kujenga dhamiri nyofu inayokumbatia upendo wa dhati, jambo ambalo ni chukizo kwa waamini wenye misimamo mikali ya kidini na wanaotaka kukumbatia vitendo vya kigaidi ili kufikia malengo yao!

Amani ni nguvu ya ndani inayoweza kuleta mabadiliko makubwa katika maisha ya mwanadamu na wala si mtutu wa bunduki: Haki na amani ni chanda na pete na kikolezo cha maendeleo endelevu yanayowahusisha binadamu wote pasi wa aina yoyote ile! Umefika wakati kwa watu kujenga utamaduni wa haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. Watu wamwongokee Mwenyezi Mungu anayesamehe na kupenda haki; mambo ambayo yanafumbatwa katika Fumbo la Maisha na Utume wa Kanisa unaopaswa kushuhudiwa kwa njia ya maisha ya Wakristo. Huu ndio ujumbe maalum wa kipindi cha Kwaresima.

Khalifa wa Mtakatifu Petro anayekabidhiwa dhamana ya kuliongoza Kanisa la Kristo anapaswa kwanza kabisa anasema Kardinali Polycarp Pengo kuwa ni Baba wa Maskini; Mtetezi wa wanyonge na wanaonyimwa na kudhulumiwa haki zao; shahidi makini wa Fumbo la Mungu lililofumbuliwa na Yesu Kristo katika historia ya maisha ya mwanadamu yanayofumbata mwanga na vivuli vya giza. Ni kipongozi anayepaswa kuwa mwema na mnyofu anayetoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao, ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo na binadamu katika ujumla wao!

Awe ni mfano mwema wa kuigwa kwa maneno na matendo yanayobubujika kutoka katika kweli za Kiinjili; ambaye yuko tayari kujikana mwenyewe bna kuubeba Msalaba wake, tayari kumfuasa Yesu, akithubutu hata kuwasamehe adui zake! Hiki ndicho kielelezo cha maisha ya Kikristo anasema Kardinali Pengo kinachohitaji toba na wongofu wa ndani.

Kuna haja kwa waamini kujikita katika kutafuta na kukumbatia yale mambo ya msingi yanayojionesha katika Fumbo la Msalaba wa Kristo, Mwana wa Mungu. Bikira Maria ni mfano na kielelezo cha Kanisa; ni mwalimu wa Ukristo na Upendo wa Kiinjili.

Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa SECAM anahitimisha mahubiri yake, kwa kumweka Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, aliyeliongoza Kanisa kwa kipindi cha miaka minane, chini ya uongozi na usimamizi wa Bikira Maria. Ni Papa aliyeliongoza Kanisa kwa uaminifu mkubwa, akatumia vyema kipaji chake cha akili na unyenyekevu. Kwa hakika anastahili kushukuriwa na kupongezwa.

Kardinali Polycarp Pengo amewaweka pia Makardinali wote wanaoshiriki katika mchakato wa kumchagua Papa Mpya chini ya uongozi na usimamizi wa Bikira Maria aliyekuwa mwanafunzi mwaminifu wa Kristo, bila woga, kiasi kwamba, wataweza kuchangia kwa dhati kabisa kumchagua yule ambaye Mwenyezi Mungu anapenda awe ni Khalifa wa Mtakatifu Petro, msingi wa umoja wa Kanisa linaloonekana. Umoja katika Mafundisho Tanzu ya Kanisa; katika Imani, Matumaini na Mapendo. Umoja katika mchakato wa kutafuta haki na amani; umoja kwa kushiriki taabu na mateso ya wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Umoja uwe ni kielelezo cha Familia ya binadamu na Muumba wao kwa kujikita katika udugu.









All the contents on this site are copyrighted ©.