2013-03-01 08:42:29

Yaliyojiri wakati Baba Mtakatifu Benedikto XVI anang'atuka madarakani!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jioni tarehe 28 Februari 2013 ameondoka rasmi kama Papa kutoka mjini Vatican, baada ya kuzungumza kwa faragha na Kardinali Tarcisio Bertone, katibu mkuu wa Vatican ambaye kwa sasa ndiye Kardinali Carmelengo, yaani "Mlinzi".

Papa alipata fursa ya kuagana na wafanyakazi wa Vatican waliofika kwa wingi wakiandamana pia na familia zao. Vikosi vya Ulinzi kutoka Uswiss vilitoa heshima zao za mwisho na baadaye Baba Mtakatifu alipanda gari kuelekea Uwanja wa Ndege wa Vatican tayari kuondoka kwenda Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo ambako kwa sasa anapumzika baada ya kulitumikia Kanisa kwa miaka minane kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Hili ni tukio ambalo limevuta hisia za watu wengi waliokuwa wamekusanyika kwanza kabisa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kushuhudia tukio hili la kihistoria lililokuwa linarushwa moja kwa moja na Kituo cha Televisheni cha Vatican hadi alipowasili kwenye Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo. Alipopita juu ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, Makao makuu ya Jiji la Roma, Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano pamoja na Makanisa kadhaa, kengele ziligonjwa kama kielelezo cha kumsindikiza Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Waamini na watu wenye mapenzi mema waliendelea kufuatilia tukio hili hadi pale ilipofika majira ya saa 2:00 Usiku, lango kuu la Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo lilipofungwa na Askari wa Kiswiss wakakabidhi dhamana ya ulinzi na usalama kwa Vikosi vya Usalama vya Vatican. Maaskari wa Kiswiss wamerudi Vatican ili kuendelea kutoa huduma yao kwa Makardinali ambao kwa sasa wako kwenye pilika pilika za kuanza mchakato wa kumchagua Papa Mpya. Ni tukio ambalo limewaacha watu wengi wakiwa wameshikwa na butwaa kwa kutoamini maamuzi magumu yaliyofanywa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita!







All the contents on this site are copyrighted ©.