2013-03-01 09:48:10

Ibada ya Kukabidhiana Msalaba wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Jimbo kuu la Dar es Salaam


Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Msalaba unachukua maana ya pekee katika maisha ya waamini, kwani wanatumwa na kuchangamotishwa kuwa ni mashahidi amini wa Kristo na Kanisa lake: kwa maneno na matendo. Msalaba ni kielelezo cha mapendo, neema, sala, msamaha na matumaini yasiyodanganya kamwe!

Ndiyo maana, Kanisa linaona fahari juu ya Msalaba wa Kristo kwa kuutembeza katika nyumba za waamini, ili wapate nafasi ya kusali na kulitafakari Fumbo la Msalaba, ishala ya mateso na alama ya wokovu wa binadamu; mahali ambapo hekima ya Mungu imetundikwa juu yake! Ni mwaliko wa kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu. Ifuatayo ni Ibada ya kukabidhiana Msalaba katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Jimbo kuu la Dar es Salaam.

Vikundi vya pande zote mbili: wanaokabdhi na waokabidhiwa wanasimama mbele ya Msalaba. Padri wa kikundi kinachokabidhi msalaba anaanza ibada:

Padri: Kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu...
Wote: Amina.
Padri: Bwana awe nanyi..
Wote: Na awe rohoni mwako.

Padri anaeleza madhumuni ya kukutana:

Padri: Ndugu zangu, tumekutana hapa ili kukabidhiana Msalaba wa Mwaka wa Imani, ambacho ni chombo alichotumia Bwana wetu Yesu Kristo kutukomboa. Tunafanya tendo hili la ibada ya kuuheshimu Msalaba ili Mungu azidi kutujalia neema ambazo Kristo alitustahilisha kwa mateso, kifo na ufufuko wake. Tunawakabidhi Msalaba huu ili muupokee kama kumpokea Kristo mwenyewe katika parokia yenu. Uwe ishara ya ujio wake Kristo katika Mwaka huu wa Imani. Wakati wote utakaokuwa parokiani kwenu utunzwe na kuheshimiwa kama chombo kitakatifu kilicholeta wokovu. Ishara ya Msalaba huu iwaletee wingi wa neema za Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu.
Wote: Amina.

Sasa tusikilize somo linalotueleza kuwa Yesu Kristo ni Mwokozi wa ulimwengu:

Somo: Yohane (3:14-21)

Inafuatia tafakari fupi

Sala za Waamini:

Padri wa kikundi kinachopokea Msalaba anaongoza Sala za Waamini:

Padri: Ndugu zangu, Yesu Kristo amemtolea Mungu Baba maisha yake Msalabani ili ampatanishe na wanadamu. Ee Baba wa huruma uyasikie maombi yetu...
Wote: Bwana utuongezee imani
    Msalaba utukumbushe mapendo makubwa ya Kristo; Msalaba uamshe shukrani mioyoni mwetu...
    Msalaba uwe bendera ya Wakristo na alama ya ushindi wao; Msalaba ututie nguvu katika mateso, vitisho na hatari...
    Msalaba utufanye tuwe imara katika imani yetu, uwe nguvu yetu ya kuwafukuza pepo wabaya na washawishi...
    Msalaba uwe nguvu yetu ya kututoa katika dhambi na mazingira ya dhambi, ili sisi sote tuweza kuingia katika ufalme wa Mungu...
    Kwa ishara ya Msalaba tuwabariki wana familia zetu; tufanye ishara ya Msalaba maishani na kifoni...

Ee Mungu, umeweka Msalaba uwe ishara ya ukombozi wetu na alama ya huruma na mapendo yako. Twakuomba utupe neema ya kuuchukua Msalaba wetu pamoja na Mkombozi kwa mapendo makubwa. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu.
Wote: Amina.

Wanakabidhiana Msalaba Mtakatifu, huku ukiimbwa wimbo ufaao...








All the contents on this site are copyrighted ©.