2013-03-01 09:14:13

Hili ni tukio la: kushangaza, kihistoria na kibinadamu! Atakumbukwa na wengi!


Rais Giorgio Napolitano wa Italia, kwa mara nyingine tena kwa niaba ya wananchi wa Italia, amemshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa upendo na mshikamano aliowaonesha wananchi wa Italia wakati wa uongozi wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni kiongozi ambaye amechangia mafao ya wengi si tu ndani ya Kanisa bali katika medani mbali mbali za maisha ya kijamii. Wengi wameonja na kuguswa na ule ukawaida wa maisha yake na kwamba, ni mtu ambaye hakupenda makuu!

Rais Nalipotano anasema, miaka minane ya uongozi wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, Vatican na Serikali ya Italia vimeweza kushirikiana kwa karibu zaidi, katika misingi ya amani na utulivu; daima kila upande ukipania kushirikiana kwa dhati kwa ajili ya mafao ya pande hizi mbili. Kwa hakika amechangia kwa namna ya pekee katika ustawi wa maisha ya kiroho kwa waamini wengi, dhamana ambayo ameitekeleza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Rais Napolitano anasema alikuwa na uhusiano wa kirafiki na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Ameonja ujasiri na moyo mkuu pale Papa alipokuwa anakabiliana na magumu katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro; lakini akaonesha pia imani, matumaini na upendo mkuu kwa Kristo na Kanisa lake, kwa maneno machache Papa Benedikto wa kumi na sita, alikuwa ni mtu wa imani thabiti. Kama viongozi, kwa pamoja waliweza kuchambua hali za maisha ya watu wao Ulaya na Duniani kwa ujumla; wakaheshimiana na kuthaminiana, hasa katika kukuza na kudumisha umoja wa kitaifa.

Rais Giorgio Napolitano anasema kwamba, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kung'atuka kutoka madarakani ni tukio la kushangaza, kihistoria na kibinadamu. Anasema, bado wataendelea kumsindikiza kwa njia ya sala katika hija ya maisha yake hapa duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.